Tuesday, September 25, 2012

KAZI KATIKA UISLAM

Uislamu Na Shari'ah Zake

UTANGULIZI

Kulingana na Kamusi ya Kiingereza ya Collins, kazi imefafanuliwa kama juhudi za kimwili au kiakili zilizoelekezwa kufanya/ kutengeneza kitu, malipo anayopewa kwa amali, biashara, utaalamu, shughuli au ufahamu.

Katika Uislam, kazi inamaanisha juhudi au uajiriwa unaofanywa ili mtu kupata pato la halali na katika mipaka ya maagizo ya Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) na kanuni Zake. Pale Muislam anapofanya hivyo kwa nia safi na ikhlasi, anapata ujira kutoka kwa Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala).

Katika Uislam dunia ni sehemu ya kuvuna kwa ajili ya Akhera. Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) Anasema:

“Na utafute, kwa Aliyokupa Allaah, makaazi ya Akhera. Wala usisahau fungu lako la dunia. Nawe fanya wema kama Allaah alivyo kufanyia wema wewe. Wala usitafute kufanya ufisadi katika ardhi. Hakika Allaah hawapendi mafisadi” (28: 77).

Na Anasema vilevile: “Na Tukaufanya mchana ni wa kuchumia maisha” (78: 11).

Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) Ametuwekea mchana hasa ili tuweze kuhangaika kimaisha.

Kwa sababu sisi tuko katika ardhi hii, Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) Ametufundisha du’aa ifuatayo ya sisi kutaka kheri za nyumba mbili. Anasema Aliyetukuka: “Na katika wao wapo wanaosema: Mola wetu Mlezi, tupe duniani mema, na Akhera mema, na utulinde na adhabu ya Moto! Hao ndio watakaopata sehemu yao kwa sababu ya yale waliyoyachuma. Na Mwenyezi Mungu ni Mwepesi wa kuhisabu” (2: 201 – 202).

Waislam katika eneo la Afrika Mashariki wanachukuliwa kuwa sawa na wavivu kwa sababu ya jinsi walivyojiweka katika hali ya uzembe wa hali ya juu. Utawaona vijana wenye miili imara wanakaa mabarabarani, kwenye mabustani na mabarazani, nje ya Msikiti na sehemu nyengine za anasa wakizembea na kuzungumza mambo ya upuuzi. Pia vijana waliohamia nchi za kimagharibi kwa sababu ya ruzuku inayotolewa na serikali wamechukua mienendo hiyo mibaya.

Si halali kwa Muislam kutofanya kazi ili kujikimu kimaisha kwa kisingizio cha kuyaweka maisha yake kuwa wakfu kwa ajili ya kufanya ‘Ibaadah au kumtegemea Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) kwa njia hiyo. Pia haifai kwao kutegemea sadaka japokuwa wana uwezo wa kufanya kazi kwa juhudi na nguvu zao. Katika hili, Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: “Sadaka si halali kwa tajiri wala mwenye uwezo wa kimwili” (at-Tirmidhiy).

Katika riwaya nyengine ya Abu Daawuud na an-Nasaa’iy, ‘Ubaydullah ibn ‘Adiyy al-Khiyaar (Radhiya Allaahu ‘anhu) ameripoti: “Watu wawili waliniambia kuwa walikwenda kwa Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) wakati wa Hijjatul Widaa alipokuwa akigawa Zakaah. Walimtaka usaidizi. Aliwatazama kuanzia utosini hadi chini na kuwaona kuwa wamejenga vizuri na wenye nguvu. Aliwaambia: ‘Ikiwa mwataka, nitawapatia (Zakaah), lakini hakuna Zakaah kwa aliye tajiri wala kwa yule mwenye nguvu anayeweza kupata pato”.

Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) aliwakataza Waislam kuomba omba pasi na dharura yoyote, hivyo kukosa heshima na hadhi. Hili lengo lake ni kuwafundisha na kuwahimiza Waislam kulinda na kuwa mbali na mienendo ya kupe kwa kuwanyonya wenziwe (watu wengine).

HADHI YA KAZI

Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) Anataja misingi inayotakiwa katika kufanya ukulima. Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) Ameitandaza ardhi na kuifanya kuwa muruwa na yenye rutuba kwa ajili ya ukulima na kumeza pamoja na kupata mazao. Zipo ayah nyingi kuhusu hilo lakini unaweza kutazama baadhi yake kwa mfano “Na ardhi Tumeitandaza na humo tumeweka milima, na tumeotesha kila kitu kwa kiasi chake. Na Tumekujaalieni humo vitu vya maisha yenu, na ya hao ambao nyinyi sio wenye kuwaruzuku. Na hakuna chochote ila asili yake inatokana na Sisi; wala hatukiteremshi ila kwa kipimo maalumu” (15: 19-22)

“Na ardhi ameiweka kwa ajili ya viumbe. Humo yamo matunda na mitende yenye mafumba. Na nafaka zenye makapi, na rehani. Basi ni ipi katika neema za Mola wenu Mlezi mnayoikanusha” (55: 10-13)

“Na Mwenyezi Mungu Amekukunjulieni ardhi kama busati. Ili mtembee humo katika njia zilizo pana.” (71: 19-20)

“Hebu mtu na atazame chakula chake. Sisi Tumemimina maji kwa nguvu, Tena Tukaipasua pasua ardhi kwa nguvu, Kisha Tukaotesha humo nafaka, Na zabibu, na mimea ya majani,” (80: 24-28) na kadhalika.

Katika ayah zote hizo kuna kuhimizwa watu kuwa wakulima na kutilia maanani ukulima. Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: “Pindi Muislam anapopanda mti au mmea, hakuna ndege wala mwanaadamu atakayekula kwayo isipokuwa anaandikiwa sadaka” (Al-Bukhaariy na Muslim).

Na katika Hadiyth nyingine anasema: “Kikisimama Qiyaama na mkononi mwa mmoja wenu ana mche akaweza kuumeza basi afanye hivyo kwani atapata ujira kwayo”. Hii ni hima ya hali ya juu aliyotupatia Mtume wetu (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) hata katika wakati mgumu kama huo wa Qiyaama ambapo mambo yote yatabadilika.

Mbali na ukulima, Muislam anaweza kujishughulisha na sayansi za msingi, viwanda na taalamu nyengine kwa idadi kubwa inayoweza kukidhi mahitaji yetu ya kijamii.

Qur-aan imetaja viwanda na taaluma nyingi na kuziita ni fadhila za Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala). Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) Anatueleza kuwa:

Nabii Daawuud (‘Alayhis Salaam) alikuwa mfua vyuma hivyo akitengeneza nguo za chuma za kivita.

“Na tukamfundisha kuunda mavazi ya vita kwa ajili yenu ili yakuhifadhini katika kupigana kwenu. Je! Mtakuwa wenye kushukuru”21: 80

“Na tulimpa Daawuuud fadhila kutoka kwetu, (tukasema): Enyi milima! Karirini kumtakasa Mwenyeezi Mungu pamoja naye! Na ndege pia. Na tukamlainishia chuma. (Tukamwambia:) Tengeneza nguo za chuma pana, na kadiria sawa katika kuunganisha. Na tendeni mema. Hakika Mimi nayaona vyema mnayo yatenda” (34: 10-11)

Nabii Sulaymaan (‘Alayhis Salaam) alikuwa mjengaji

“Na Sulaymaan tuliufanya upepo umtumikie. Safari yake ya asubuhi ni mwendo wa mwezi mmoja, na safari yake ya jioni ni mwendo wa mwezi mmoja. Na tukamyayushia chemchem ya shaba. Na katika majini walikuwako walio kuwa wakifanya kazi mbele yake kwa idhini ya Mola wake Mlezi. Na kila anayejitenga na amri yetu katika wao, tunamwonjesha adhabu ya Moto unaowaka. Walikuwa wakimfanyia alipendalo, kama mihrabu, na masanamu, na madeste makubwa kama mahodhi, na masufuria makubwa yasiyo ondolewa mahala pake. Enyi watu wa Daawuud! Fanyeni kazi kwa kushukuru. Ni wachache katika waja wangu wanao shukuru” (34: 12-13),

Dhul Qarnayn alitengeneza ukuta mrefu kama kizuizi dhidi ya maadui

“Akasema: Yale Mola wangu aliyo niwezesha ni bora zaidi. Lakini nyinyi nisaidieni kwa nguvu zenu. Nitakujengeeni kizuizi baina yenu na wao. Nileteeni vipande vya chuma. Hata alipo ijaza nafasi iliyo kati ya milima miwili, akasema: Vukuteni. Hata alipo kifanya (chuma) kama moto akasema: Nileteeni shaba iliyo yayuka niimwagie. Basi hawakuweza kuukwea, wala hawakuweza kuutoboa” (18: 95-97)

Nabii Nuuh (‘Alayhis Salaam) alikuwa seremala

“Na unda jahazi mbele ya macho yetu na kwa mujibu wa ufunuo wetu. Wala usinisemeze kuwatetea walio dhulumu. Kwani hao bila ya shaka watazamishwa. Na akawa anaunda jahazi, na kila wakipita wakuu wa kaumu yake wakimkejeli. Yeye akasema: Ikiwa nyinyi mnatukejeli na sisi tunakukejelini kama mnavyo tukejeli” (11: 37-38).

Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) pia Anatutajia merikebu kubwa sana kama milima, ambazo zinavuka baharini

“Na katika Ishara zake ni vyombo vinavyo kwenda na kurejea baharini kama vilima” (42: 32).

Zaidi ya hayo, Qur-aan imetufahamisha kuwa chuma kina thamani kwa kutilia mkazo jambo hilo.

Anasema Aliyetukuka: “Kwa hakika tuliwatuma Mitume wetu kwa dalili waziwazi, na tukateremsha Kitabu pamoja nao na Mizani, ili watu wasimamie uadilifu, na tumeteremsha chuma chenye nguvu nyingi na manufaa kwa watu, na ili Mwenyezi Mungu Amjue anaye mnusuru Yeye na Mitume wake kwa ghaibu” (57: 25).

Kazi yoyote yenye kukidhi mahitaji ya jamii au inayoleta faida ya kihakika inachukuliwa kuwa ni nzuri, ilimradi anayeifanya aifanye kwa njia nzuri, kama inavyotakikana na Uislam. Baadhi ya watu wanazitweza baadhi ya kazi, lakini Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) anatufundisha kuwa heshima na hadhi ya mtu imefungamana na yeye kufanya kazi – kazi aina yoyote ila zile zilizo haramishwa. Hivyo, Uislam ulinyanyua hadhi na vyeo vya kazi nyingi ambazo watu walikuwa wanaziona kuwa duni.

Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: “Ni bora kwa mtu kuchukua kamba na kuleta mzigo wa kuni mgongoni mwake na kuzuiza ili Allaah Ailinde heshima yake, kuliko yeye kuomba kutoka kwa watu bila kujali kama watampatia au watamnyima” (al-Bukhaariy na Muslim).

Ndio yule Swahaba alipokariri kuja kumtaka msaada Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam), Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alimuuliza kama ana akiba yoyote nyumbani kwake. yule bwana akamwambia anacho kitambara. Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alimwagizia akilete, na kilipoletwa alikinadi nacho kikanunuliwa kwa dinari mbili. Moja kati ya hizo dinari mbili Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alimwambia anunulie chakula na akiache nyumbani. Ya pili Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) mwenyewe alikwenda sokoni na kununua kile chuma cha shoka na kumtilia mpini kwa mkono wake. Kisha alimwambia asionekane pale mpaka baada ya muda fulani. Swahaba huyo alielekea msituni ili kukata kuni. Baada ya muda Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alikutana na huyo bwana kukiwa na sauti ya pesa zikilia mfukoni kwake. Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alimwambia hii ni bora kabisa kuliko kuomba omba.

Mitume na Manabii (‘Alayhimus Salaam) ndio ruwaza njema kwetu. Wao walifanikiwa katika kazi zao kwa kiasi kikubwa. Ibn ‘Abbaas (Radhiya Allaahu ‘anhuma) amesema: “Daawud alikuwa mtengenezaji makoti ya chuma na ngao zake, Aadam alikuwa mkulima, Nuuh alikuwa seremala, Idriys mshonaji na Muusa mchungaji” (Al-Haakim).

Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: “Allaah Hakumtuma Mtume bila ya yeye kuchunga kondoo”. Wakamuuliza Maswahaba: “Hata wewe, ewe Mtume wa Allaah?” Akajibu: “Hata mimi, nilikuwa nikichunga kondoo wa watu wa Makkah kwa ujira” (Al-Bukhaariy).

Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) aliwaambia Maswahaba zake hivi ili kuwafunza kuwa heshima inakuwa kwa wale wanaofanya kazi, na sio wale wenye kukaa na kuzembea na kuwa kupe kuwala wengine. Nasi tunaakiwa tufuate mtindo huo wa kufanya kazi. Zipo fursa nyingi, ambazo zinaonekana na sisi Waislam kama ni kazi duni zinazotuteremsha vyeo ambapo wengi wanaishi kwa kufanya kazi hizo na vile vile kuwa na hadhi zao nzuri. Na hivyo kuwa na heshima na hakuna wa kumkebehi au kumdharau kwa kuwa yeye anafanya juhudi na anakula kwa jasho lake.

Uislam umetuhimiza sisi kufanya biashara, na kuziita kutafuta fadhila ya Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala). Tafadhali tazama ayah zifuatazo kuhusu mas-ala hayo 2: 198; 24: 37; 28: 57; 73: 20 na kadhalika.

Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: “Mfanya biashara muaminifu atakuwa pamoja na Manabii, wakweli na mashahidi” (At-Tirmidhiy na al-Haakim). Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) mwenyewe aliweka nidhamu kabambe na kanuni za kibiashara mbali na ghushi (udanganyifu), kuwasilisha kwa namna nyengine, kuficha bidhaa na kufanyiana hiyana.

Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) ametupigia mfano wa jinsi ndege anavyofanya juhudi kutafuta riziki na akakuita kuwa ni kumtegemea Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) katika hilo. Hivyo kumtegemea Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) ni mwanzo kumfunga ngamia kisha kumuomba Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) asimfanye atoroke. Imepokewa kwa ‘Umar ibn al-Khatwtwaab (Radhiya Allaahu ‘anhu) kuwa amemsikia Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) akisema: “Ikiwa nyinyi mtamtegemea Allaah upeo wa kumtegemea basi Atawaruzuku nyinyi kama Anavyomruzuku ndege. Anatoka katika kiota chake asubuhi tumbo lake likiwa tupu na anarudi ikiwa tumbo lake limejaa” (At-Tirmidhiy, Ahmad na Ibn Maajah na Isnadi yake ni Sahihi).

KAZI ZILIZOHARAMISHWA

Uislam umeharamisha baadhi ya kazi, ambazo zinakwenda kinyume na kiini cha misingi yake. Ni haramu kumeza, kula au kuvuta mti kama hashiysh, tumbaku, marijuana, na mihadarati mingineyo ambayo ni haramu kuliwa, kutafunwa au kuvutwa, kwa kuwa mimea kama hiyo haina matumizi mengine ila ya kuleta madhara. Pia si sababu sahihi kwa Muislam kusema anapanda miti au anafuga wanyama kwa ajili ya kuwauzia wasiokuwa Waislam, kwani Muislam haruhusiwi kushiriki katika kueneza vilivyo haramu na vyenye madhara.

Uislam pia umekataza taalamu fulani na viwanda kwa wafuasi wake kwa sababu zina madhara kwa itikadi, maadili, heshima, muruwa na kadhalika. Mfano ni kama ukahaba ambao Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) Anasema: “Wala msiwashurutishe vijakazi vyenu kufanya zinaa kwa ajili ya kutafuta pato la maisha ya dunia, ilhali wao wanataka kujihishimu. Na atakaye walazimisha basi Allaah baada ya kulazimishwa kwao huko, Atawasamehe, kwani Allaah ni Mwenye kusamehe, Mwenye kurehemu” (24: 33).

Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) pia alikataza hilo, bila kuangalia wala kujali nani atafaidika kwayo. Uislam umekataza dansi, muziki hata nyimbo zenye kuamsha hisia za kiume au kike au shughuli nyingine yoyote kama hiyo, kama nyimbo zenye kuashiria au zilizo chafu au michezo ya kuigiza yenye kuelekeza kwenye uasherati na kadhalika. Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) Anasema: “Wala msikaribie uzinzi. Hakika huo ni uchafu na njia mbaya” (17: 32).

Utengenezaji wa vileo, mihadarati na masanamu pia umeharamishwa. Uislam umekataza biashara yenye dhulma, udanganyifu, kuongeza faida kubwa sana katika biashara au kueneza vitu vya haramu. Pia ni haramu kufanya biashara ya pombe, nguruwe, masanamu au kitu chengine chochote ambacho utumiaji wake umeharamishwa na Uislam. Wafanya biashara wawe na tahadhari ya kughushi, kugeuza au kuvuruga vipimo na ratili, kuzuilia na kuficha bidhaa ili asiwe ni mwenye kukosa ulinzi wa Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala). Pia atahadhari kwa hilo, kwani Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) Anasema yafuatayo kuhusu kupunja katika kupima: “Ole wao hao wapunjao! Ambao wanapojipimia kwa watu hudai watimiziwe. Na wao wanapowapimia watu kwa kipimo au mizani hupunguza” (83: 1-3).

Watu wa Madyan, waliotumiwa Mtume Shu‘ayb (‘Alayhis Salaam) ili kuwaonya dhidi ya kupunja wanapopima waliadhibiwa vikali sana na Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) baada ya kumkadhibisha Nabii wao (Tazama 7: 85-93 na 11: 84-95).

Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) Anatoa onyo kali kwa mwenye kuchukua na kutoa riba na Ametangaza vita dhidi yao.

Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) Anasema: “Enyi mlio amini! Mcheni Mwenyeezi Mungu, na acheni riba zilizobakia, ikiwa nyinyi ni Waumini, Basi mkitofanya jitangazieni vita na Mwenyeezi Mungu na Mtume Wake. Na mkitubu, basi haki yenu ni rasilmali zenu. Msidhulumu wala msidhulumiwe” (2: 278-279).

Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: “Dirhamu moja ya riba ambayo mtu ataitumia kwa kujua ni mbaya zaidi kuliko kufanya zinaa mara 36” (Ahmad).

Haifai kabisa kuficha vyakula ili kupata faida nyingi zaidi au kuficha kasoro ya bidhaa yoyote unayouza.

SIFA NZURI ZA MFANYAKAZI MUISLAM

Mfanyakazi Muislam mzuri ana sifa maridhawa zifuatazo:

1. Mjuzi na Mwenye Elimu: Ujuzi na elimu ni sifa muhimu sana ili shughuli zote ziendeshwe kitaalamu kama inavyotakiwa. Ndio Nabii Yuusuf (‘Alayhis Salaam) alimwambia mfalme wa Misri yafuatayo: “Yusuuf akasema: Nifanye mshika khazina za nchi. Kwani hakika mimi ni mlinzi mjuzi” (12: 55).

2. Uaminifu na Nguvu: Allaah (Subhaanahu wa Ta‘ala) Anazungumzia kuhusu tazkiya aliyotoa binti ya mzee mkongwe kwa babake kwa sifa alizokuwa nazo Muusa (‘Alayhis Salaam): “Akasema mmoja katika wale wanawake: Ewe baba yetu! Muajiri huyu. Hakika mbora wa kumuajiri ni mwenye nguvu na muaminifu” (28: 26).

Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: “Mfanyabiashara muaminifu atakuwa pamoja na Manabii, wakweli na mashahidi” (At-Tirmidhiy na al-Haakim). Muislam ni lazima awe muaminifu katika shughuli zake zote na kutokuwa muaminifu ni kuwa na moja wapo wa alama ya unafiki.

3. Kutunza Vitu vilivyo chini yake: Allaah (Subhaanahu wa Ta‘ala) Anamzungumzia Nabii Yuusuf (‘Alayhis Salaam) pale aliposema: “Nifanye mshika khazina za nchi. Kwani hakika mimi ni mlinzi mjuzi” (12: 55).

4. Bidii na Juhudi: Pato la kufanya kwa mikono yako ndio kazi bora kabisa ambayo mtu anaweza kufanya. Imepokewa na Rafi‘ ibn Khadij (Radhiya Allaahu ‘anhu) kuwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) aliulizwa ni pato gani lililo bora zaidi, naye akajibu: “Ni mtu kufanya kazi kwa mikono yake na kila biashara iliyokubaliwa (na sheria)” (Ahmad na at-Tirmidhiy).

Mitume wote (‘Alayhimus Salaam) walikuwa wakila kwa pato la jasho lao kwa kufanya kazi.

5. Kutunza Wakati wa Kazi: Hii ni sifa ya Muumini aliyejikita katika Iymaan. Mtu anapoanza kazi huwa ana mkataba na mkubwa wa kampuni au shirika na kila mfanyakazi huwa ana masaa yake ya kuwa kazini. Kutotekeleza hilo huwa unajiingiza katika sifa ya unafiki kwani Muislam mwema na mzuri ni yue anayetunza mkataba na ahadi.

SIFA NZURI ZA MWAJIRI MUISLAM

Mwajiri Muislam ni lazima afikirie na azingatie zile hisia za wanaadamu wenziwe. Hivyo, asimtwike mwajiriwa kwa kumpatia kazi au mzigo asiouweza. Tazama jinsi gani yule mzee mkongwe na mcha Mungu alivyomwambia Nabii Muusa (‘Alayhis Salaam): “Akasema: Mimi nataka kukuoza mmojawapo katika binti zangu hawa wawili kwa kunitumikia miaka minane. Ukitimiza kumi, khiari yako; lakini mimi sitaki kukutaabisha. InshaAllaah utanikuta miongoni mwa watu wema” (28: 27).

Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema yafuatayo kuhusu hayo kama ilivyopokewa na Safwaan kutoka kwa Maswahaba wa Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) kwamba amesema: “Tahadharini sana, kwani yeyote atakayemdhulumu mtu aliyeandikiana naye mkataba, au akampunja haki yake, au akamlazimisha kufanya kazi ngumu upeo wa nguvu zake, au akamchukulia chochote pasi na idhini yake, mimi nitamtetea Siku ya Qiyaama” (Abu Daawuud).

Mwajiri hafai kumtwika mzigo mkubwa hata mtumwa wake kwa kumpatia kazi zaidi ya uwezo wake, basi mwajiriwa ndio haifai zaidi. Imepokewa kwa Abu Hurayrah (Radhiya Allaahu ‘anhu) kuwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: “Ni muhimu sana kumlisha mtumwa, kumvisha (sawa sawa) na kutomtwika mzigo wa kupita uwezo wake” (Muslim).

Katika riwaya ya Imaam Maalik, Abu Hurayrah (Radhiya Allaahu ‘anhu) amepokea kuwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: “Mtumwa anafaa apatiwe chakula na mavazi kwa njia ya kawaida, na anawajibika kufanya zile kazi anazoweza bila ya shida”. Maalik amesema kuwa ‘Umar ibn al-Khatwtwaab (Radhiya Allaahu ‘anhu) alikuwa akienda vijijini kila siku ya Jumamosi na pindi anapomuona mtumwa anafanya kazi inayopita uwezo na nguvu zake basi alikuwa akimpunguzia.

Mfanyakazi anatakiwa alipwe ujira au mshahara wake kikamilifu pindi tu anapomaliza kazi yake hiyo au mwisho wa mwezi. Kuhusu hili amepokea Abu Hurayrah (Radhiya Allaahu ‘anhu) kuwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: “Hapana, lakini mfanyakazi analipwa ujira wake kamili pale tu anapomaliza kazi yake” (Ahmad na at-Tirmidhiy). Na katika riwaya nyengine: “Kabla jasho lake halijakauka”.

Allaah (Subhaanahu wa Ta‘ala) Anamchukia na Atakuwa dhidi ya mwajiri asiyelipa ujira au mshahara kwa ukamilifu kwa waajiriwa wake. Imepokewa kwa Abu Hurayrah (Radhiya Allaahu ‘anhu) kuwa Mtume wa Allaah (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: “Allaah Anasema: ‘Nitakuwa dhidi ya watu watatu Siku ya Qiyaama:

1. Mtu anayefanya ahadi kwa jina Langu, lakini anafanya khiyana,

2. Mtu anayemuuza mtu huru (kama mtumwa) na kula thamani yake, na

3. Mwajiri anayemwandika kibarua ambaye anafanya kazi yake kiukamilifu lakini yeye hamlipi ujira wake’” (Al-Bukhaariy).

HITIMISHO

Kwa muono wa Uislam, Waumini wa kweli ni wale wenye kutekeleza amali na kutia bidii katika kazi zao za halali, ambao sifa zao za kipekee ni kuwa shughuli za hii dunia haziwafanyi wao kusahau wajibu wao kwa Mola wao Mlezi. Allaah (Subhaanahu wa Ta‘ala) Anasema: “Watu ambao biashara wala kuuza hakuwashughulishi na kumdhukuru Allaah, na kushika Swalah, na kutoa Zakaah. Wanaikhofu Siku ambayo nyoyo na macho yatageuka” (24: 37).

Muislam mzuri ni yule ambaye baada ya amali yoyote ya ‘Ibaadah moja anajitupa uwanjani ili kutafuta fadhila za Allaah (Subhaanahu wa Ta‘ala). Allaah (Subhaanahu wa Ta‘ala) Anasema: “Na itakapo kwisha Swalah, tawanyikeni katika nchi mtafute fadhila za Allaah, na mkumbukeni Allaah kwa wingi ili mpate kufanikiwa” (62: 10). Allaah (Subhaanahu wa Ta‘ala) kwa hima na sisitizo Alilotupatia kwa kazi Hakuiacha hata siku tukufu na siku kuu ya wiki, Ijumaa iwe sisi hatufanyi kazi bali Anataka baada ya Swalah ya Ijumaa tutawanyike katika ardhi ili tufanye kazi na tupate riziki ya halali.

Muislam anapotunukiwa fadhila na Allaah (Subhaanahu wa Ta‘ala), anafaa amuhimidi na kumshukuru Muumba wake kwa kushikilia amri Zake na kukaa mbali na makatazo Yake. Huu ni mtihani kutoka kwa Allaah (Subhaanahu wa Ta‘ala), kwani Yeye Anasema: “Haya ni katika fadhila zake Mola wangu Mlezi, ili anijaribu nitashukuru au nitakufuru. Na mwenye kushukuru, kwa hakika, anashukuru kwa manufaa ya nafsi yake; na anaye kufuru, kwa hakika Mola wangu Mlezi ni Mkwasi na Karimu” (27: 40).

Lau waajiri Waislam watachukua maagizo haya na kujipamba na sifa tulizozitaja zilizowekwa na Allaah (Subhaanahu wa Ta‘ala) na Mtume Wake (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) na waajiriwa nao wakatekeleza wajibu na majukumu yao basi hakungekuwa na matatizo aina yoyote katika jamii yetu ya Kiislam. Inabidi sisi turudi katika Uislam sahihi uliokamilishwa na Mtume wetu, Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) ili tupate kufanikiwa hapa duniani na kesho Akhera.

Friday, August 10, 2012

Laylatul-Qadr- Vipi Uweze Kuupata Usiku Huu?

Tunaingia kumi la mwisho, kumi ambalo ndani yake kuna siku tukufu, siku ya Laylatul-Qadr, ambayo ibada yake ni bora kuliko ibada ya miezi elfu.

Anasema Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala):

﴿ بِسْمِ اللّهِ الرَّحْمَنِ الرَّحِيمِ ﴾ (( إِنَّا أَنزَلْنَاهُ فِي لَيْلَةِ الْقَدْرِ)) (( وَمَا أَدْرَاكَ مَا لَيْلَةُ الْقَدْرِ)) (( لَيْلَةُ الْقَدْرِ خَيْرٌ مِّنْ أَلْفِ شَهْرٍ)) ((تَنَزَّلُ الْمَلَائِكَةُ وَالرُّوحُ فِيهَا بِإِذْنِ رَبِّهِم مِّن كُلِّ أَمْرٍ)) (( سَلَامٌ هِيَ حَتَّى مَطْلَعِ الْفَجْرِ ))

BismiLlaahir Rahmaanir Rahiym

((Hakika Sisi Tumeiteremsha Qur-aan katika Laylatul Qadr, (Usiku wa Makadirio[Majaaliwa]). Na nini kitachokujuulisha nini Laylatul Qadr?)) ((Laylatul-Qadr ni bora kuliko miezi elfu)) ((Huteremka Malaika na Roho (Jibriyl) katika usiku huo kwa idhini ya Mola wao kwa kila jambo)) ((Amani usiku huo mpaka mapambazuko ya alfajiri)) [Al-Qadr: 1-5]

Vile vile dalili katika Hadiyth mbali mbali zimethibiti kuhusu Fadhila za usiku huu mtukufu, na jinsi Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) alivyokuwa hali yake katika siku hizi kumi za mwisho za Ramadhaan.

Baada ya kuzijua fadhila zake usiku huu mtukufu inakupasa Muislamu ujikaze katika siku kumi hizi za mwisho kuacha mambo yote yanayokushughulisha ya dunia na utumbukie katika ibada tu ili uweze kuupata usiku huo mtukufu, yaani ukukute wewe ukiwa katika ibada ili zihesabiwe ibada zako kama kwamba umefanya ibada ya miezi elfu.

Tukifanya hesabu miezi elfu hiyo ni sawa na umri wa miaka 83!

1000 ÷ 12 = 83.3 yaani miaka themanini na tatu na miezi mitatu takriban.

Hivyo ikiwa Laylatul-Qadr imekukuta katika ibada ya aina yoyote, ikiwa ni Swalah (Qiyaamul-Layl), kusoma Qur-aan, kufanya aina za dhikr, kutoa sadaka, kulisha chakula, kuwasiliana na jamaa, kujielimisha au kuelimisha, kufanya wema kwa watu, yote hayo utaandikiwa kama umefanya hayo kwa umri wa miaka 83! Na juu ya hivyo ibada hiyo ya usiku mmoja tu ni bora zaidi kuliko ibada utakayoweza kufanya miaka 83 na miezi mitatu. Subhaana Allaah!

Jihadhari ndugu Muislamu usije ukakukuta usiku huu mtukufu ukiwa katika maasi au katika sehemu ukiwa umeghafilika na ya dunia kama sokoni, magenge ya soga au michezo ya kupoteza wakati au kwenye televisheni ukiangalia misalsalaat, mipira na sinema zikakupita kheri zote za usiku huu. Utaona siku hizi Waislamu wengi wanashughulika kwenda madukani kutafuta nguo za 'Iyd khaswa kina dada wakiacha masiku haya yawapite wakiwa humo badala ya kuwa majumbani mwao au misikitini kufanya ibada na kutegemea kuupata usiku huu.

Ni siku chache tu ndugu Waislamu ambazo zinakimbia kama upepo. Je, nani basi katika sisi atakayepuuza asiupate usiku huo? Na Nani katika sisi atafanya hima kuupata usiku huo? Kwani hatujui kama tutakuweko duniani mwakani kuzipata siku hizi au hata hatujui kama tutaikamilisha Ramadhaan hii. Basi tujitahidi kwa kukesha siku kumi hizi na kuamsha familia zetu ili iwe kheri yetu kukutana na usiku huo mtukufu tuweze kupata fadhila zake hizo ambazo ni sawa na kulipwa malipo ya umri mrefu kama tulivyoona hapo nyuma hata kama hatutoruzukiwa umri huo.

Mwenye Kuukosa Usiku Huu Amekula Khasara Kubwa

Hakika mwenye kuukosa usiku huo atakuwa amenyimwa kheri zake na itakuwa ni khasara kuukosa usiku huu mtukufu kama anavyosema Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam):

عَنْ أَبِي هُرَيْرَة رَضِيَ اللَّه عَنْهُ قَالَ : لَمَّا حَضَرَ رَمَضَان قَالَ رَسُول اللَّه صَلَّى اللَّه عَلَيْهِ وَسَلَّمَ (( قَدْ جَاءَكُمْ شَهْرُ رَمَضَان شَهْرٌ مُبَارَكٌ اِفْتَرَضَ اللَّهُ عَلَيْكُمْ صِيَامَهُ تُفْتَح فِيهِ أَبْوَاب الْجَنَّة وَتُغْلَق فِيهِ أَبْوَابُ الْجَحِيم وَتُغَلُّ فِيهِ الشَّيَاطِين فِيهِ لَيْلَة خَيْرٌ مِنْ أَلْف شَهْر مَنْ حَرُمَ خَيْرهَا فَقَدْ حُرِمَ)) وَرَوَاهُ النَّسَائِيّ

Kutoka kwa Abu Huraryah (Radhiya Allaahu 'anhu) kwamba ilipofika Ramadhaan, amesema Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam): ((Umekujieni mwezi wa Ramadhaan, ni mwezi wa Baraka. Imefanywa Swawm kwenu kuwa ni Fardh, milango ya Pepo hufunguliwa na milango ya moto hufungwa na mashaytwaan hufungwa. Umo katika mwezi huu usiku ulio bora kuliko miezi elfu. Atakayenyimwa kheri zake hakika kanyimwa haswa)) [An-Nasaaiy]

Siku hiyo ni siku iliyoteremeshwa Qur-aan kutoka mbingu ya saba hadi mbingu ya kwanza kama Anavyosema Allaah (Subhaanahu Wa Ta'ala):

﴿ بِسْمِ اللّهِ الرَّحْمَنِ الرَّحِيمِ ﴾ ((حم)) ((وَالْكِتَابِ الْمُبِينِ)) (( إِنَّا أَنزَلْنَاهُ فِي لَيْلَةٍ مُّبَارَكَةٍ إِنَّا كُنَّا مُنذِرِينَ)) ((فِيهَا يُفْرَقُ كُلُّ أَمْرٍ حَكِيمٍ))

BismiLlaahir Rahmaanir Rahiym

((Haa Miym)) ((Naapa kwa Kitabu kinachobainisha)) ((Hakika Tumekiteremsha katika usiku uliobarikiwa. Hakika Sisi ni Waonyaji)) ((Katika usiku huu hubainishwa kila jambo la hikima)) [Ad-Dukhaan: 1-4]

Aya ya nne inayosema 'Katika usiku huu hubainishwa kila jambo la hikma' kuwa kuna makadirio ya mwaka huo na yote yatakayotokea katika mwaka mzima. Kwa maana kwamba, siku ya Laylatul-Qadr, makadirio yote yaliyomo katika Al-Lawhum-Mahfuudhw (Ubao uliohifadhiwa) na huteremshwa haya makadirio na Malaika ambao wanaandika makadirio ya mwaka unaokuja yakiwa ni kuhusu umri wetu wa kuishi, rizki zetu, na yatakayotokea yote hadi mwisho wake. [Imesimuliwa na Ibn 'Umar, Mujaahid, Abu Maalik, Adh-Dhwahaak na wengineo katika Salaf – Ibn Kathiyr: 8:671]

Kujikaza kufanya ibada

Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) alikuwa inapoingia kumi la mwisho akijikaza kwa kufanya ibada kuliko siku zozote zingine:

عن عائشة – رضي الله عنها- قالت: " كان رسول الله – صلى الله عليه وسلم- يجتهد في العشر الأواخر، ما لا يجتهد في غيره" مسلم

Kutoka kwa Mama wa Waumini 'Aaishah (Radhiya Allaahu 'anha) kwamba: "Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alikuwa akijitahidi katika kumi la mwisho kuliko alivyojitahidi katika siku nyingine zozote" [Muslim]

Na katika Swahiyhayn (Al-Bukhaariy na Muslim):

عن عائشة رضي الله عنها، قالت: "كان رسول الله صلى الله عليه وسلّم إذادخل العشر شذ مئزره، وأحيا ليله، وأيقظ أهله ( وفي رواية) "أحيا الليل،وأيقظ أهله، وجدّ، وشدّ المئزر" رواه البخاري ومسلم،.

Kutoka kwake pia Mama wa Waumini 'Aaishah (Radhiya Allaahu 'anha): "Ilipokuwa inaingia kumi (la mwisho) Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) alikaza izaar (shuka) yake, akikesha usiku, na akiamsha ahli zake" (Na katika riwaaya nyingine) "Akikesha usiku, akiamsha ahli zake, akijitahidi na akikaza izaar yake" [Al-Bukhaariy na Muslim]

Kwa Nini Umeitwa Laylatul-Qadr?

Amesema Shaykh Ibn 'Uthaymiyn (Rahimahu-Llaah):

Kwanza: Kutokana na uwezo nao ni utukufu kama vile kusema “fulani mwenye uwezo mkubwa" yaani mwenye hadhi au utukufu.

Pili: Ni usiku ambao una makadirio ya mwaka mzima na huandikwa yote yatakayotokea mwaka huo, na hii ni Hikma ya Allaah (Subhaanahu Wa Ta'ala) na kuonyesha usanifu wa utengenezaji Wake na Uumbaji Wake.

Tatu: Usiku huo una uwezo mkubwa kama alivyosema Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam):

من قام ليلة القدر إيمانا واحتسابا غفر له ما تقدم من ذنبه)) متفق عليه

((Atakayesimama usiku wa Laylatul-Qadr kwa iymaan na kutaraji malipo, ataghufuriwa madhambi yake yaliyotangulia)) [Al-Bukhaariy na Muslim]

Sababu Ya Kupewa Waislamu Laylatul-Qadr

Sababu ya kupewa Ummah huu wetu wa Kiislamu siku hii tukufu ya Laylatul-Qadr ni kwamba:

Mtume (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) aliona umri wa Ummah za mwanzo ni mrefu, na umri wa Ummah wake ni mfupi akapewa usiku wa Laylatul-Qadr uwe ni bora kuliko miezi elfu. [Muwatwtwaa 1/321 (Muhammad Fuad 'Abdul-Baaqy]

Ibada Za Kufanya Masiku Kumi Haya Katika Kukesha

1-Qiyaamul-Layl:(Kisimamo cha usiku kuswali)

((من قام رمضان إيماناً واحتساباً غفر له ما تقدم من ذنبه)) متفق عليه

((Atakayesimama (Kuswali) Ramadhaan kwa iymaan na kutaraji malipo, ataghufuriwa madhambi yake yaliyotangulia)) [Al-Bukhaariy na Muslim]

2-Kuosma Qur-aan

Khaswa kwa vile usiku wa Laylatul-Qadr ndio usiku ulioteremeshwa Qur-aan kama tulivyoona katika Aayah hizo za juu katika Suratul-Qadr na Suratud-Dukhaan.

Vile vile Ramadhaan nzima inampasa Muislamu asome Qur-aan kwani ni mwezi ulioteremshwa Qur-aan kama Anavyosema Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala):

((شَهْرُ رَمَضَانَ الَّذِيَ أُنزِلَ فِيهِ الْقُرْآنُ هُدًى لِّلنَّاسِ وَبَيِّنَاتٍ مِّنَ الْهُدَى وَالْفُرْقَانِ))

((Mwezi wa Ramadhaan ambao imeteremshwa humo Qur-aan kuwa ni uongofu kwa watu, na hoja zilizo wazi za uongofu na upambanuzi)) [Al-Baqarah: 185]

Na Jibriyl ('Alayhis-Salaam) alikuwa akimteremkia Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) kila usiku wa Ramadhaan akimsomesha na kumsikiliza Qur-aan:

"كَانَ رَسُولُ اللَّهِ -صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ- أَجْوَدَ النَّاسِ وَكَانَ أَجْوَدُ مَا يَكُونُ فِي رَمَضَانَ حِينَ يَلْقَاهُ جِبْرِيلُ وَكَانَ يَلْقَاهُ فِي كُلِّ لَيْلَةٍ مِنْ رَمَضَانَ فَيُدَارِسُهُ الْقُرْآنَ" رواه البخاري

Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) alikuwa ni mbora (mwenye matendo mema) wa watu, na alikuwa mbora zaidi katika Ramadhaan kwa sababu Jibriyl alikuwa akimjia kila usiku wa Ramadhaan akimfundisha Qur-aan)) [Al-Bukhaariy]

3- I'tikaaf

Kutia nia kubakia msikitini kwa kufanya ibada tu humo kwani Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) alikuwa akifanya hivyo:

عن عائشة – رضي الله عنها- قالت "كان النبي يعتكف في كل رمضان عشرة أيام؛ فلما كان العام الذي قبض فيه اعتكف عشرين يوماً - أخرجه البخاري

Kutoka kwa Mama wa Waumini 'Aaishah (Radhiya Allaahu 'anha) kwamba: Mtume (swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) alikuwa akifanya I'tikaaf kila Ramadhaan siku kumi, ulipofika mwaka wake wa kuaga dunia alifanya I'tikaaf siku ishirini" [Al-Bukhaariy]

4-Kuomba Maghfirah

Kwani usipoghufuriwa madhambi yako basi ni hatari!

عَنْ أَنَس وَغَيْره أَنَّ النَّبِيّ صَلَّى اللَّه عَلَيْهِ وَسَلَّمَ لَمَّا صَعِدَ الْمِنْبَر ثُمَّ قَالَ (( آمِينَ آمِينَ آمِينَ)) " قِيلَ يَا رَسُول اللَّه عَلَامَ مَا أَمَّنْت ؟ قَالَ (( أَتَانِي جِبْرِيل فَقَالَ يَا مُحَمَّد رَغِمَ أَنْف رَجُل ذُكِرْت عِنْده فَلَمْ يُصَلِّ عَلَيْك قُلْ آمِينَ فَقُلْت آمِينَ ثُمَّ قَالَ رَغِمَ أَنْف رَجُل دَخَلَ عَلَيْهِ شَهْر رَمَضَان ثُمَّ خَرَجَ فَلَمْ يُغْفَر لَهُ قُلْ آمِينَ فَقُلْت آمِينَ ثُمَّ قَالَ رَغِمَ أَنْف رَجُل أَدْرَكَ وَالِدَيْهِ أَوْ أَحَدهمَا فَلَمْ يُدْخِلَاهُ الْجَنَّة قُلْ آمِينَ فَقُلْت آمِينَ )) صحيح الترمذي و قال الشيخ الأباني حسن صحيح

Kutoka kwa Anas na wengineo kwamba Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) alipopanda juu ya minbar aliitikia ((Aamiyn, Aamiyn, Aamiyn)). Alipoulizwa kwa nini ameitikia hivyo akasema: ((Amenijia Jibriyl akasema: Ewe Muhammad, ole wake yule ambaye unapotajwa hakuswalii, hivyo sema Aamiyn. Nikasema Aamiyn. Kisha akasema: ole wake yule ambaye umeingia mwezi wa Ramadhaan kisha akatoka bila ya kughufuriwa, kwa hiyo sema Aamiyn. Nikasema Aamiyn. Kisha akasema: ole wake yule ambaye amewakuta wazazi wake au mmoja wa wazazi wake lakini wasimuingize Peponi. Hivyo sema Aamiyn. Nikasema Aamiyn)) [Swahiyh At-Tirmidhiy na kasema Shaykh Al-Albaaniy kuwa Hadiyth hiyo ina daraja ya Hasan Swahiyh]

5-Du'aa Ya Kuomba Maghfirah Katika Siku Kumi Hizi Zakaatul-Fitwr Mwisho

عن عائشة رضي الله عنها أنها قالت يا رسول الله أرأيت إن وافقت ليلة القدر ما أدعو قال: ((تقولين: اَللَّهُمَّ إِنَّكَ عَفُوٌ تُحِبُّ الْعَفْو فَاعْفُ عَنِّي)) ابن ماجه و صححه الألباني Kutoka kwa mama wa waumini bibi 'Aaishah (Radhiya Allaahu 'anha) kwamba alisema "Ewe Mjumbe wa Allaah je, nitakapowafikiswha usiku wa Laylatul-Qadr niombe nini?" Akasema, ((Sema: Ewe Allaah Hakika Wewe Ndiye Mwenye Kusamehe Unapenda Kusamehe basi Nisamehe)) [Ibn Maajah na kaisahihisha Al-Albaaniy]

Matamshi Yake

Allaahumma Innaka 'Afuwwun Tuhibbul-'Afwa Fa'afu 'Anniy

6-Kumkumbuka Allaah Kwa Aina Zozote Za Dhikr

Kwa Tasbiyh, Tahmiyd, Tahliyl, Takbiyr (kusema: Subhaana Allaah, Alhamdulillah, Laa Ilaaha Illa Allaah, Allaahu Akbar)

7- Kuomba Du'aa Na Haja Zako

Kwa vile ni mwezi wa kuomba Du'aa pia kwani Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala Ameunganisha Aayah za kufaridhishwa Swawm na Aaya za kuhusu kuomba Du'aa:

((وَإِذَا سَأَلَكَ عِبَادِي عَنِّي فَإِنِّي قَرِيبٌ أُجِيبُ دَعْوَةَ الدَّاعِ إِذَا دَعَانِ فَلْيَسْتَجِيبُواْ لِي وَلْيُؤْمِنُواْ بِي لَعَلَّهُمْ يَرْشُدُونَ))

((Na waja Wangu watakapokuuliza khabari Zangu, waambie kuwa Mimi nipo karibu. Naitikia maombi ya mwombaji anaponiomba. Basi na waniitikie Mimi, na waniamini Mimi, ili wapate kuongoka)) [al-Baqarah: 186]

Usiku Gani Khaswa Unapatikana Laylatul-Qadr?

Hadiyth zimetaja siku kadhaa ambazo usiku huu mtukufu hutokea katika siku kumi za mwisho na haswa katika usiku wa witiri, zikiwa zimetajwa nyingine kuwa ni usiku wa siku ya ishirini na moja, au ishirni na tatu, au ishirni na tano au ishirini na saba kama ilivyokuja katika dalili zifuatazo:

لحديث عائشة أن رسول الله صلى الله عليه وسلم قال: ((تحروا ليلة القدر في الوتر من العشر الأواخر)) رواه البخاري

Hadiyth kutoka Mama wa Waumini 'Aiashah (Radhiya Allaahu 'anha) kwamba Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: ((Utafuteni usiku wa Laylatul-Qadr katika siku za witiri kwenye siku kumi za mwisho)) [Al-Bukhaariy]

وفي حديث ابن عباس رضي الله عنهما أن النبي صلى الله عليه وسلم قال: (( التمسوها في العشر الأواخر من رمضان ليلة القدر في تاسعة تبقى ، في سابعة تبقى ، في خامسة تبقى)) رواه البخاري

Hadiyth kutoka Ibn 'Abbaas (Radhiya Allaahu 'anhuma) kwamba Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: ((Utafuteni usiku wa Laylatul-Qadr katika siku kumi za mwisho za Ramadhaan, katika (usiku wa) tisa, saba, na wa tano utakaobakia [mwisho wa Ramadhaan])) [al-Bukhaariy]

Imaam Ahmad amerikodi kutoka kwa 'Ubaydah bin As-Swaamit kwamba alimuuliza Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) kuhusu usiku wa Laylatul-Qadr akasema:

((فِي رَمَضَان فَالْتَمِسُوهَا فِي الْعَشْر الْأَوَاخِر فَإِنَّهَا فِي وِتْر إِحْدَى وَعِشْرِينَ أَوْ ثَلَاث وَعِشْرِينَ أَوْ خَمْس وَعِشْرِينَ أَوْ سَبْع وَعِشْرِينَ أَوْ تِسْع وَعِشْرِينَ أَوْ فِي آخِر لَيْلَة ))

((Katika Ramadhaan, utafuteni siku kumi za mwisho, hakika umo katika siku za witiri, siku ya ishirini na moja, au ishirini na tatu, au ishirini na tano, au ishirini na saba, au ishirini na tisa, au usiku wa mwisho)) [Ahmad]

Alama Zinazobainisha Laylatul-Qadr

1. Kwenye usiku huo kunakuwa na mwanga zaidi. 2. Upepo siku hiyo hutulia, yaani siku hiyo hautokei upepo mkali. 3. Hali ya hewa huwa nzuri. 4. Nyoyo siku hizo huwa na utulivu na unyenyekevu zaidi kuliko siku nyingine. 5. Baadhi ya watu wema huoteshwa usiku kama walivyokuwa wakioteshwa Maswahaba na Salafus-Swaalih (wema waliotangulia)

Asubuhi Yake

حديث أبي بن كعب رضي الله عنه أنه قال : "أخبرنا رسول الله صلى الله عليه وسلم أنها تطلع يومئذ ٍ لا شعاع لها" رواه مسلم

Hadiyth kutoka kwa Ubay bin Ka'ab (Radhiya Allaahu 'anhu) kwamba: "Ametuambia Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) kuwa jua hutoka siku hiyo likiwa halina mishale (mikali)" [Muslim]

(( ليلة القدر ليلة طلقة لا حارة ولا باردة ، تُصبح الشمس يومها حمراء ضعيفة)) صحيح ابن خزيمة

((Laylatul-Qadr usiku ulio katika hali ya ukunjufu, usio na baridi wala joto, asubuhi yake jua huwa jekundu na dhaifu)) [Swahiyh Ibn Khuzaymah]

ليلة القدر ليلة بلجة (أي مضيئة) لا حارة ولا باردة ، لا يرمى فيها بنجم)) (أي لا ترسل فيها الشهب) رواه الطبراني ومسند أحمد

((Laylatul-Qadr usiku wa kung'aa [yaani wenye mwanga] sio joto wala baridi, na vimondo (nyota za kufyatuliwa) hazitotumwa)) [At-Twabaraaniy na Ahmad]

Tunamuomba Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) Atuwezeshe kukesha masiku haya kumi ili tujaaliwe kuupata usiku huu mtukufu tutoke katika Ramadhaan hii tukiwa tumeghufuriwa madhambi yetu yote na tumepewa fadhila za usiku huu mtukufu zinazolingana na kuongezewa umri wa miaka 83. Aamiyn

Nasiha Za Minasaba Mbalimbali http://www.alhidaaya.com

Friday, July 20, 2012

Nyakati Tatu Muhimu Za Kufanya Ibada – Zisikupite Katika Ramadhaan

Nasiha Za Minasaba Mbalimbali

www.alhidaaya.com

Nyakati tatu hizi ni muhimu sana za kufanya ibada kutokana na fadhila zake kuu. Mwenye kupenda kuchuma thawabu nyingi asizikose khaswa katika mwezi huu Mtukufu Wa Ramadhaan ambao ni mwezi wenye malipo maradufu

1-Wakati wa mwanzo: Baina ya Alfajiri na jua kuchomoza:

Usimulizi uliothibiti kutoka katika Swahiyh Muslim (564/1) kwamba Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na Maswahaba walikuwa wakibakia macho wakati huo hadi jua kuchomoza kwani ni wakati mja anapogaiwa rizki yake, na ni wakati wenye kheri nyingi, unampa siha nzuri ya mwili binaadamu, na kwa ujumla ni wakati wenye baraka nyingi za kila aina kwani Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) aliomba:

((اللهم بارك لأمتي في بكورها)) الترمذي, أحمد, أبي داود, ابن ماجه

((Ewe Allaah, wabarikie Ummah wangu nyakati za asubuhi mapema)) [At-Tirmidhiy, Ahmad, Abu Daawuud, Ibn Maajah na imethibitishwa kuwa ni Hadiyth Swahiyh na Shaykh Al-Albaaniy]

Usimulizi huu umetoka kwa Maswahaba kadhaa ambao wameelezea kwamba: "Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) alipotaka kupeleka kikosi au jeshi aliwapeleka mwanzo wa asubuhi". Vile vile wamesimulia kwamba: "Swakhar alikuwa mtu tajiri ambaye alikuwa akipelekea biashara zake mwanzo wa asubuhi na matokeo yake ilikuwa ni kufuzu katika biashara na kupata faida kubwa sana".

Wamesimulia Salafus-Swaalih kwamba Ibn 'Abbaas naye alimkataza mtu kulala nyakati hizo alipomwambia:

"قُم، أتنام في الساعة التي تقسَّم فيه الأرزاق؟"

"Inuka! Je, unalala katika saa ambayo rizki inagaiwa?"

Ikiwa basi wakati huo ni kama hivyo ilivyoelezwa juu, basi vipi Muislamu auache wakati huu umpite khaswa katika mwezi huu mtukufu wa Ramdhaan?

Ibnul-Qayyim (Rahimahu-Allaah) katika kitabu chake 'Zaad Al-Ma'aad' amesema: "Usingizi wa asubuhi unanyima rizki kwani huo ni wakati ambao Muumba anaombwa rizki na wakati wa kugaiwa rizki. Hivyo usingizi unanyima rizki isipokuwa kwa dharura. Usingizi wakati huo pia ni madhara kwa mwili…"

Faida nyingine kubwa ya kubakia macho ukimdhukuru Allaah wakati huu:

Si chini ya muda wa saa na nusu utakuwa umepata thawabu za Hajj na ‘Umrah kamilifu:

عن أنس عن النبي صلى الله عليه وسلم ، أنه قال (( من صلى الفجر في جماعة ثم قعد يذكر الله حتى تطلع الشمس ثم صلى ركعتين كانت له كأجر حجة وعمرة تامة تامة تامة) ) أخرج الترمذي صححه الألباني .

Imetoka kwa Anas kwamba Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: ((Atakayeswali Alfajiri katika Jama'ah kisha akakaa anamkumbuka Allaah mpaka likachomoza jua kisha akaswali Raka'ah mbili, atapata ujira kama ujira wa kwenda Hajj na 'Umrah ulio kamili kamili kamili)) [Imetolewa na At-Tirmidhiy na kaisahihisha Al-Albaaniy]

Pindi ukifanya hivyo kwa mwezi mzima utakuwa umechuma thawabu za Hajj na ‘Umrah mwezi mzima. Hizo ni fadhila za siku za kawaida, seuze ukifanya mwezi mtukufu huu wa Ramadhaan? Jitahidi ndugu Muislamu kadiri uwezavyo kuchuma hizi thawabu kubwa ambazo zingelikukalifu mali, tabu za safari na mashaka ya kufika Makkah kutekeleza ibada hizo. Lakini kwa Rahma ya Allaah Ametujaalia tuweze kuzichuma tukiwa majumbani mwetu tena kwa wepesi kabisa. Wanaume thawabu zitazidi ikiwa watatekeleza wakiwa misikitini. Wanawake wanazipata fadhila hizo hata wakiswali majumbani mwao. Hata hivyo, pamoja na ujira wote huu, tusisahau kuwa fadhila hizo hazivunji wala hazifuti fardh ya kwenda Hajj kwa mwenye uwezo, asije mtu akadhani kufanya hayo kutakuwa kumetengua wajiibu wake wa kuhiji au kufanya ‘Umrah.

2- Wakati wa pili: Kabla ya Jua kuzama (Magharibi):

Huu ni wakati ambao bado Muislamu yuko katika Swawm na du'aa yake anayoiomba hairudi:

قال صلى الله عليه وسلم: ((ثلاثة لا ترد دعوتهم: الصائم حتى يفطر والإمام العادل والمظلوم)) وروى الترمذي بسند حسن

Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: (([Watu] watatu du'aa zao hazirudi; mwenye kufunga hadi afuturu/afutari, Kiongozi muadilifu na aliyedhulumiwa)) [At-Tirmidhiy kwa isnaad nzuri]

Kwa hiyo ni fursa ya kuitumia Muislamu aombe du'aa na haja zake wakati huu khaswa pia kwa vile ni wakati ambao Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) Amehimiza Atukuzwe kama Anavyosema:

(( وَسَبِّحْ بِحَمْدِ رَبِّكَ قَبْلَ طُلُوعِ الشَّمْسِ وَقَبْلَ الْغُرُوبِ)) ((.. na mtakase kwa kumsifu Mola wako kabla ya kuchomoza jua na kabla ya kuchwa)) [Qaaf: 39]

((وَسَبِّحْ بِحَمْدِ رَبِّكَ قَبْلَ طُلُوعِ الشَّمْسِ وَقَبْلَ غُرُوبِهَا وَمِنْ آنَاء اللَّيْلِ فَسَبِّحْ وَأَطْرَافَ النَّهَارِ لَعَلَّكَ تَرْضَى))

((…Na umtakase Mola wako kwa kumsifu kabla ya kuchomoza jua, na kabla halijachwa, na nyakati za usiku pia umtakase, na ncha za mchana ili upate ya kukuridhisha)) [Twaahaa: 130].

(( وَاسْتَغْفِرْ لِذَنبِكَ وَسَبِّحْ بِحَمْدِ رَبِّكَ بِالْعَشِيِّ وَالْإِبْكَار))

((…Na omba msamaha kwa dhambi zako, na umtakase Mola wako kwa kumhimidi jioni na asubuhi)) [Ghaafir: 55]

3- Wakati wa tatu: Suhuur - Kabla ya Alfajiri

Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) Amewaaahidi Wacha Mungu Pepo kwa sababu sifa mojawapo yao ni kuomba maghfira kabla ya Alfajiri:

إِنَّ الْمُتَّقِينَ فِي جَنَّاتٍ وَعُيُون)) ((آخِذِينَ مَا آتَاهُمْ رَبُّهُمْ إِنَّهُمْ كَانُوا قَبْلَ ذَلِكَ مُحْسِنِينَ)) ((كَانُوا قَلِيلًا مِّنَ اللَّيْلِ مَا يَهْجَعُونَ)) ((وَبِالْأَسْحَارِ هُمْ يَسْتَغْفِرُون))

((Hakika wenye taqwa watakuwa katika Mabustani na chemchem)) ((Wanapokea Aliyowapa Mola wao. Kwa hakika hao walikuwa kabla ya haya wakifanya mema)) ((Walikuwa wakilala kidogo tu usiku)) ((Na kabla ya Alfajiri wakiomba maghfira)) [Adh-Dhaariyaat: 15-18]

Kisha wamesifiwa tena kwa sifa hiyo hiyo pamoja na nyinginezo:

((الصَّابِرِينَ وَالصَّادِقِينَ وَالْقَانِتِينَ وَالْمُنفِقِينَ وَالْمُسْتَغْفِرِينَ بِالأَسْحَارِ))

((Wanaosubiri, wanaosema kweli, na watiifu, na wanaotoa sadaka, na wanaoomba maghafira kabla ya Alfajiri)) [Al-'Imraan: 17]

Muislamu asiache wakati huo umpite kwani ni wakati muhimu na wenye fadhila na faida kubwa kwa vile Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) Huteremka wakati huo kutoka mbingu ya saba na kuweko mbingu ya ardhi kutukidhia haja zetu:

عن أبي هريرة رضي الله عنه أن رسول الله صلى الله عليه وسلم قال: ((ينزل ربنا تبارك وتعالى كل ليلة إلى السماء الدنيا حين يبقى ثلث الليل الآخر فيقول: من يدعوني فأستجيب له؟ من يسألني فأعطيه؟ من يستغفرني فأغفر له )) البخاري و مسلم

Imetoka kwa Abu Hurayrah (Radhiya Allaahu 'anhu) kwamba Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: (Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) Huteremka (kwa namna inavyolingana na utukufu Wake) kila siku katika mbingu ya dunia (mbingu ya kwanza) inapobakia thuluthi ya mwisho ya usiku na Husema: Nani ananiomba Nimtakabalie? Nani ana shida Nimtekelezee? Nani ananiomba maghfirah Nimghufurie?)) [Al-Bukhaariy na Muslim]

Nani miongoni mwetu asiyemhitaji Mola wake kumkidhia haja zake na kumuondeshea shida zake? Nani asiyekuwa na madhambi asiyemhitaji Mola wake kumghufuria? Hivyo usiache wakati huu ukakupita khaswa kwa vile mwezi huu Mtukufu ambao kila jambo ulifanyalo lina fadhila na thawabu marudufu.

Tunamuomba Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) Atuwezeshe kudiriki nyakati hizo tatu na nyingine, tuwe katika ibada katika mwezi huu wa Ramadhaan na miezi yote mingineyo na Atujaalie kheri na Baraka nyingi, Atukidhie haja zetu, Atuondoshee shida zetu na Atughufurie madhambi yetu yote. Aamiyn.

Thursday, July 12, 2012

Njia 10 Za Kuukaribisha Vizuri Mwezi Mtukufu Wa Ramadhaan

Nasiha Za Minasaba Mbalimbali Anasema Allaah سبحانه وتعالى: ((يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُواْ كُتِبَ عَلَيْكُمُ الصِّيَامُ كَمَا كُتِبَ عَلَى الَّذِينَ مِن قَبْلِكُمْ لَعَلَّكُمْ تَتَّقُونَ)) (( أَيَّامًا مَّعْدُودَاتٍ فَمَن كَانَ مِنكُم مَّرِيضًا أَوْ عَلَى سَفَرٍ فَعِدَّةٌ مِّنْ أَيَّامٍ أُخَرَ وَعَلَى الَّذِينَ يُطِيقُونَهُ فِدْيَةٌ طَعَامُ مِسْكِينٍ فَمَن تَطَوَّعَ خَيْرًا فَهُوَ خَيْرٌ لَّهُ وَأَن تَصُومُواْ خَيْرٌ لَّكُمْ إِن كُنتُمْ تَعْلَمُونَ)) ((شَهْرُ رَمَضَانَ الَّذِيَ أُنزِلَ فِيهِ الْقُرْآنُ هُدًى لِّلنَّاسِ وَبَيِّنَاتٍ مِّنَ الْهُدَى وَالْفُرْقَانِ فَمَن شَهِدَ مِنكُمُ الشَّهْرَ فَلْيَصُمْهُ وَمَن كَانَ مَرِيضًا أَوْ عَلَى سَفَرٍ فَعِدَّةٌ مِّنْ أَيَّامٍ أُخَرَ يُرِيدُ اللّهُ بِكُمُ الْيُسْرَ وَلاَ يُرِيدُ بِكُمُ الْعُسْرَ وَلِتُكْمِلُواْ الْعِدَّةَ وَلِتُكَبِّرُواْ اللّهَ عَلَى مَا هَدَاكُمْ وَلَعَلَّكُمْ تَشْكُرُونَ)) ((Enyi mlioamini! Mmefaradhishiwa Swawm, kama waliyofaradhishiwa waliokuwa kabla yenu ili mpate kumcha Allaah))(([Mfunge] siku maalumu za kuhisabika. Na atakayekuwa miongoni mwenu mgonjwa au yumo safarini basi atimize hisabu katika siku nyengine. Na wale wasioweza, watoe fidiya kwa kumlisha masikini. Na atakayefanya wema kwa kujitolea, basi ni bora kwake. Na mkifunga ni bora kwenu, kama mnajua)) ((Mwezi wa Ramadhaan ambao imeteremshwa humo Qur-aan kuwa ni uongofu kwa watu, na hoja zilizo wazi za uongofu na upambanuzi. Basi atakayekuwa mjini katika mwezi huu na afunge. Na mwenye kuwa mgonjwa au safarini, basi atimize hisabu katika siku nyengine. Allaah Anakutakieni yaliyo mepesi wala Hakutakieni yaliyo mazito, na mtimize hiyo hisabu, na mumtukuze Allaah kwa kuwa Amekuongoeni ili mpate kushukuru)) [Al-Baqarah: 183-185] Inatupasa tumshukuru Allaah سبحانه وتعالى kwa Kutujaalia uhai na afya mpaka tunakaribia kufika mwezi mtuku wa Ramadhaan na hii ni fursa nyingine Anayotupa katika maisha yetu kushuhudia mwezi huu na kupata fadhila zake. Na hii ni neema ya Allaah سبحانه وتعالى Ambaye Ametujaalia kuwa na miezi iliyo bora kuliko miezi mingine au siku bora au masaa bora kuliko mengine, ambazo thawabu zake za mema yanayotendeka humo huwa ni zaidi ya nyakati nyingine. Mfano wake ni kama kunapokuwa na mauzo yaliyopunguzwa bei dukani (sale), ambayo kawaida yake huwekwa kwa muda mdogo tu maalum. Na muda huu mtu huweza kununua vitu vingi kwa malipo kidogo tu. Hali kadhalika Ramadhaan, ni mwezi mmoja tu, lakini malipo yake huwa ni mengi kuliko hata malipo ya miezi yote mingine. Ikiwa mtu atatimiza Swawm yake inavyopaswa na kufanya mema mengi, na akawa katika Twa'a (utiifu) kamili na kuomba maghfira, basi hutoka katika mwezi huu akiwa ameghufuriwa madhambi yake. Amesema Mtume صلى الله عليه وآله وسلم : (( من صام رمضان إيماناً واحتساباً ، غفر له ما تقدم من ذنبه )) أخرجه البخاري ومسلم ((Atakayefunga Ramadhaan kwa iymaan na kutaraji malipo, ataghufuriwa madhambi yake yaliyotangulia)) [Al-Bukhaariy na Muslim] Ramadhaan ni mwezi ambao tunatimiza Fardhi mojawapo ya Kiislamu. Ni mwezi uliojaa baraka, kheri na Rahma za Allaah سبحانه وتعالى. Kila Muislamu inampasa aukaribishe mwezi huu kwa furaha na matumaini kamili. Zifuatazo ni njia kumi za kujitayarisha kuukaribisha mwezi wa Ramadhaan na kupata manufaa makubwa pindi utakapotimiza: 1. Du'aa Anza kwa kuomba Du'aa kwamba mwezi huu ukufikie wakati umo katika hali ya siha nzuri na usalama hata uweze kufunga na kufanya ibada zako kwa hamu kubwa na wepesi. 2. Mazoezi katika mwezi wa Sha'abaan Funga Sunnah nyingi katika mwezi wa Sha'abaan, soma Qur-aan Juzuu moja kila siku au chini yake, amka usiku uswali japo Raka'ah mbili, kisha zidisha kidogo kidogo hadi inapoingia Ramadhaan uwe tayari umeshapata mazoezi mazuri. 3. Shukurani Mshukuru Allaah سبحانه وتعالى Kukupa uhai na siha hata uifikie Ramadhaan nyingine. Imaam An-Nawawy alisema, kwamba shukurani inapasa kwa kila jambo jema unalojaaliwa kubwa au dogo na vile vile shukurani inapasa kwa kila jambo baya Analokuepusha nalo Allaah سبحانه وتعالى. Kwa hivyo fanya 'Sajdatush-Shukr' [Sajda ya kumshukuru Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala)] kwa neema hii tukufu. 4. Furaha Furahia kukufikia mwezi wa Ramadhaan kama unavyomfurahikia mgeni mpenzi anapokuja kwako na kumuandalia mazuri yote. Maswahaba رضي الله عنهم, walikuwa wakiamkiana unapoingia mwezi wa Ramadhaan na Mtume صلى الله عليه وآله وسلم alikuwa akisema hivi anapowapa habari nzuri za mwezi wa Ramadhaan: ((جاءكم شهر مبارك افترض عليكم صيامه تفتح فيه أبواب الجنة وتغلق فيه أبواب الجحيم وتغل فيه الشياطين فيه ليلة خير من ألف شهر من حرم خيرها فقد حرم)) رواه أحمد ((Umekujieni mwezi wa Ramadhaan, ni mwezi wa Baraka. Imefanywa Swawm kwenu kuwa ni Fardh, milango ya Pepo hufunguliwa na milango ya moto hufungwa na mashaytaan hufungwa. Umo katika mwezi huu usiku ulio bora kuliko miezi alfu. Atakayenyimwa kheri zake hakika kanyimwa [yote ya kheri] )) [Ahmad] 5. Jipangie wakati na weka maazimio Ni jambo la kusikitisha kuona watu wengi wanafurahia kuingia mwezi wa Ramadhaan kwa kujiandaa kupanga mambo ya kidunia badala ya mambo ya Akhera. Wengi hukimbilia kwenda sokoni kununua nguo za 'Iyd, na kufurahikia vipindi vya Ramadhaan katika televisheni ambavyo sio vya dini kama 'misalsal' (maonyesho ya sinema yanayoendelea [series]), na pia kuanza kukusanya video za filamu, mipira, na mambo ya kupotezea muda usiku wa Ramadhaan. Pia wengine kunua karata, dhumna, meza ya mchezo wa keram kwa maandalizi ya vipumbazo na vipoteza muda katika mchana wa Ramadhaan ili wasiihisi Swawm au kuupeleka muda haraka kama wanavyoamini wao. Badala ya kufanya maandalizi ya kununua misahafu ya ziada, kanda za mawaidha, Qur-aan, kukusanya video za mawaidha na mafunzo mbalimbali ya Dini, vitabu vya Dini kwa lugha wanayoifahamu kwa wepesi na kadhalika. Huu ni mwezi wa kufanya ibada na fursa ya kujichumia mema mengi yamfaayo mtu Akhera. Kwa hiyo ndugu Waislamu, tujitahidi kuutumia wakati wetu wote bila ya kupoteza hata dakika moja, na muhimu sana kujipangia mapema wakati wako kama ifuatavyo: Ni bora kujipangia nyakati zote za mwezi mzima vipi utatumia muda wako wa mchana na usiku. Weka maazimio ya dhati kuchukua fursa kamili ya wakati wote wa mwezi huu. Weka mpango maalum wa kazi zako hata uweze kuswali kwa wakati kila kipindi, kusoma Qur-aan, kula daku na mengineyo kama tutakavyotaja hapa chini. Kama ni mwanafunzi na kama unakuwa ukisoma usiku, lala mapema, kisha uamke uswali Qiyaamul-Llayl na usome masomo yako baada ya hapo. Anza mpango wako kwa siku chache na kama unahitaji kurekebisha kuboresha nidhaam yako fanya hivyo uweze kujua nidhaam ipi itakayowafikiana na hali yako. Nasaha kwa kina Mama na kina Dada: Fanyeni maandalizi mapema ya kununua vyakula vya mwezi wa Ramadhaan na kuviandaa vyenye kuandalika mapema kabla Ramadhaan haijaanza, kama vile; sambusa, madonge ya chapati, maji ya matunda n.k. na kuweka kwenye mashine ya kugandisha barafu (freezer) au jokofu ili ikifika Ramadhaan muwe na kazi chache za jikoni na muweze kupata nafasi kubwa ya kushughulika na Ibaadah mbalimbali kama kusoma Qur-aan, kusikiliza mawaidha na hata kuhudhuria Darsa za Dini. 6. Tawbah na Maghfirah Omba Tawbatun-Nasuuha kwa Mola wako na waombe msamaha wale uliowakosea. Kufanya hivi kutanufaisha zaidi Swawm na Swalah zako na pia kukupa imani kuwa huna haki ya mtu. 7. Jifunze Fiqhi ya Swawm Jifunze elimu ya mambo yanayohusu Swawm (Fiqhi ya funga), hiyo ni muhimu ili usije kufanya jambo la kuharibu Swawm yako. Jifunze Swawm kama aliyokuwa akifunga Mtume صلى الله عليه وآله وسلم ndio mfano bora kabisa wa kuufuata. Swawm haifunguliwi kwa kula na kunywa tu, bali pia ni kujiepusha na maneno mabaya na kufanya mambo mabaya kama kusengenya, kutukana, kugombana. Mtume صلى الله عليه وآله وسلم amesema: ((من لم يدع قول الزور والعمل به والجهل فليس لله حاجة في أن يدع طعامه وشرابه)) البخاري ((Yeyote asiyeacha kusema maneno mabaya? Na vitendo vibaya basi hana haja kuacha chakula chake na maji)) [Al-Bukhaariy] 8. Jitayarishe kuchuma mema mengi Mwezi wa Ramadhaan ni mwezi wa ukarimu, huruma, rahma na mapenzi. · Panga kabisa na kuweka kiwango fulani cha kutoa Sadaka na kutoa kwa maskini, anzia kwanza kwa ndugu na jamaa. · Kama inakupasa kutoa Zakah, na umependa iwe katika mwezi wa Ramadhaan fanya hima uitimize Fardhi hii pia. · Weka 'azma ya kufuturisha kwa kualika ndugu, jamaa, jirani na marafiki kwani kumfuturisha mtu ni thawabu. ((قال صلى الله عليه وسلم : من فطر صائماً كان له مثل أجره غير أنه لا ينقص من أجر الصائم شيء)) أخرجه أحمد والنسائي وصححه الألباني ((Amesema Mtume صلى الله عليه وآله وسلم "Atakayemfutarisha aliyefunga, atapata ujira kama ujira wake bila ya kupungua chochote katika ujira wa yule aliyefunga)) [Ahmad, An-Nasaaiy na kasahihisha Imaam Al-Albaaniy] · Kama unaye jirani asiye Muislamu, mjulishe kuhusu Ramadhaan, faida na Fadhila zake. Hii ni njia na fursa mojawapo ya kufanya da'awah kwa jirani yako. 9. Hitimisha Qur-aan, Hifadhi na jifunzeTarjama Jipangie wakati uweze kuhitimisha Qur-aan kwani Ramadhaan ndio mwezi ulioteremshwa Qur-aan na hii ni Sunnah aliyokuwa akifanya Jibriyl عليه السلام kwa Mtume صلى الله عليه وآله وسلم kusoma naye Qur-aan yote ((عن ابن عباس رضي الله عنهما قال: "كان رسول الله صلى الله عليه وسلم أجود الناس، وكان أجود ما يكون في رمضان حين يلقاه جبريل، وكان يلقاه في كل ليلة من رمضان فيدارسه القرآن؛ ((رواه البخاري ((Kutoka kwa Ibn 'Abbaas رضي الله عنهما kwamba: Mtume صلى الله عليه وآله وسلم alikuwa ni mbora (mwenye matendo mema) wa watu, lakini alikuwa mbora zaidi katika Ramadhaan kwa sababu Jibriyl alikuwa akimjia kila usiku wa Ramadhaan akimfundisha Qur-aan)) [Al-Bukhaariy] Hadiyth hii inatufundisha yafuatayo: Kusoma Qur-aan katika Ramadhaan; Kukutana kwa ajili hiyo; Kupima hifdh yako ya Qur-aan kwa kukaa na Mwalimu au mwenye elimu nzuri ya Qur-aan kwa kukusikiliza au kukufundisha; Kuongeza juhudi za kusoma Qur-aan zaidi katika mwezi wa Ramadhaan: Katika muda wa masaa 24 weka saa moja au mbili khaswa iwe ya Qur-aan kusoma na kujifunza maana ya maneno ya Mola wako uonje ladha ya Qur-aan. Vile vile jitahidi kujiwekea wakati wa kuhifadhi japo sura ndogo ili ukitoka katika Ramadhaan uwe una surah zaidi za kusoma katika Swalah zako. 10. Darsa Hudhuria Darsa katika mwezi huu au soma vitabu vya dini, au sikiliza mawaidha. Jambo hili ni muhimu sana kwani kusikiliza mawaidha ni njia muhimu na bora kabisa katika kuzidisha imani yako. Kwa hakika unahitaji saa tu kuweza kutimiza jambo hili muhimu kila siku. Kama huwezi kuhudhuria msikitini, Alhamdulillah, ALHIDAAYA imewatayarishia mawaidha mengi ya kusikiliza na ya VIDEO. Kwa hiyo badala ya kutazama televisheni na kusikiliza muziki jambo ambalo ni haramu ni bora utazame na kusikiliza mawaidha ujipatie manufaa, thawabu na kuongeza elimu yako. Kumbuka kwamba kama vile mwili unavyohitajia chakula, hali kadhalika Moyo na Nafsi zinahitaji chakula chake nacho ni kumkumbuka Allaah سبحانه وتعالى kwa kila aina ya ukumbusho, na mawaidha na darsa za dini ni mojawapo ya chakula kizuri kabisa cha kutakasa Moyo na Nafsi kwa kuzijaza iymaan na mapenzi ya Mola Wako Mtukufu. Kwa kumalizia, tunasema: Fungua 'Swafha' (Ukurasa) mpya katika maisha yako Baada ya kuweza kuyatimiza hayo yote, bila ya shaka hali yako ya iymaan imekuwa bora kabisa na utakuwa umejibadilisha na kuwa mtu tofauti na ulivyo. Kwa hivyo weka maazimio ya kuendelea hata baada ya Ramadhaan kuwa katika twa'a na ibada, na kuendeleza Qiyaamul-Layl (Swalah za usiku), kusoma Qur-aan japo kidogo KILA SIKU, na iwe umefungua UKURASA MPYA wa maisha yako na kumuomba Allaah سبحانه وتعالى Akuendeleze katika hali hii. Tunachukua Fursa hii ya kuwaombeeni Ramadhaan yenye baraka na kheri nyingi, tutoke katika mwezi huu tukiwa tumesafishwa madhambi yetu yote, na wenye kubeba thawabu nyingi ziwe nzito katika Miyzaan ya Hasanaat (mizani ya amali njema) Siku ya Qiyaamah. اللَّهُمَّ تَقَبَّلْ مِنّأ وَ مِنْكُم صَالح الأّعْماَل Allaahumma Taqabbal Minnaa wa Minkum Swaalih al-A'amaal. Aamiyn

Friday, June 15, 2012

Mungu Wao Ni Mpira

Zingatio La Wiki 'Abdun-Naaswir Hikmany Iwapo mwanaadamu anataka kuonekana mtu wa maajabu, basi aseme kwamba hana ushabiki wa mpira wala sie mfuasi wa timu yoyote. Hapo uwanja wa stihzai, lawama na matusi utafunguliwa dhidi yake. Kwa hakika mpira ni mfumo mwengine wa maisha, kwani ina ratiba yake na ushabiki wake ni kinyume kabisa na mfumo mzima wa Kiislamu. Tunapozungumzia mpira hatumaanishi yale mazoezi ambayo wanaume wengi wanayafanya. Hapa tunazungumza kuhusiana na mechi ambazo vijana kwa wazee wanazifuatilia kuliko hata Qur-aan na Sunnah yake. Ingawa kwa upande fulani hayo mazoezi ya mpira nayo pia yana walakin, kwani kivazi chake ni cha utupu, mazoezi yanafanywa hadi wakati wa Swalaah na kituko chengine ni kuwepo timu za wanawake. Muislamu atambue kuwa mwenye kuamini muongozo wa asiyekuwa Mtume Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) na akaitakidi kwamba huo ndio muongozo ulio kamili kuliko muongozo wa Mtume, basi mtu huyo ni kafiri. Halikadhalika, ratiba za mpira haswa klabu za Uingereza na timu za taifa za Ulaya ni zenye kuzishughulisha akili za Waislamu. Akili ambazo zinashindwa kuhifadhi ya maana zikadumazwa kwa majina ya wachezaji na historia zao. Basi tambua kwamba kuikataa na kuipa mgongo diyn ya Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) na ukawa hujifunzi chochote katika diyn ni kutoka nje ya Uislamu. Naye Anasema Muumba wa Mbingu na Ardhi: {{Na ni nani dhalimu zaidi kuliko yule aliyekumbushwa Aayah za Mola wake kisha akazikataa. Hakika Sisi ni wenye kuchukua kisasi kwa watu wabaya.}} [As-Sajdah: 22] Kwaweza kuwa na ukweli fulani katika burudani hiyo ya mpira kwamba Muislamu hana starehe nyengine zaidi ya hiyo. Na kwa wapenzi wa mpira wanasema ni bora kuliko ushabiki wa pombe ama uzinifu. Hayo yametolewa na mashabiki wa mpira. Tunawaambia kwamba hakuna kitu chochote katika dunia hii ambacho ni kibaya kwa asilimia mia moja. Kila kitu kina madhara na manufaa yanayohusiana nacho. Hata hivyo, mtazamo wa Sharia’h ya Kiislamu, pamoja na mambo mengine, unajumuisha kupima uzito wa faida na hasara za vitu. Kwani tumeshuhudia kuwa ligi za mpira zina madhara mengi kuliko manufaa. Hii ni kwa dalili ya Tamko Lake Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala): {{Sema: “katika hivyo, mna madhara makubwa na manufaa kwa baadhi ya watu. Lakini madhara yake ni makubwa zaidi kuliko manufaa yake.”}} [Al-Baqarah: 219] Miongoni mwa madhara makubwa ya mpira ni kuwafanya Waislamu kurukwa na akili ikawa hata kutoleana salamu ni kazi ngumu kabisa. Utawakuta kwenye vigenge na hata kazini wakizozana kuhusu mechi hizo. Katika maajabu makubwa ni pale mshabiki wa mpira ambaye ni kijana wa miaka 29 alipoamua kujidhulumu nafsi yake kwa kujinyonga huko Embakasi, Nairobi – Kenya mnamo tarehe 06/05/09. Kisa na mkasa? Ati timu yake imeshindwa! Kiroja kikubwa ni kwamba hiyo mechi wenyewe ilichezwa Uingereza hali ya kuwa yeye yupo Kenya. Kama si wazimu ni nini?! Ni vyema Waislamu wakatafuta ya maana kuliko kupotezewa muda wao katika mambo yasiyokuwa na manufaa yoyote. Sio kaburini wala siku ya Hisabu ambayo Muislamu ataulizwa: "Ni ipi timu yako" au "Nitajie wachezaji wawili wa timu fulani na historia zao." Hilo halipo, isipokuwa jitayarishe na masuala haya: "Nani Mola wako" na "Nani Mtume wako". Na iwapo hayo masuala ni mepesi basi endelea kufanya istihzai na diyn yako uyaone ya mtema kuni. Tunamuomba Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) Atuongoze katika njia sahihi na Atughufurie madhambi yetu.

Thursday, June 7, 2012

Qur-aan Maana, Majina na Kuteremshwa Kwake

NINI MAANA YA QUR-AAN? 

Qur-aan ni maneno ya Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala)   yaliyoletwa kama 'Wahyi' (Ufunuo) kwa Mjumbe wa Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) na Mtume wa mwisho Muhammad (Swalla Allahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) yaliyoandikwa katika Misahafu, yanayorithiwa na vizazi kwa vizazi, yaliyonukuliwa kwa mapokezi mengi, kusoma kwake ni ibaada, ni yenye miujiza hata kama ni sura ndogo kabisa, na ni uongofu kamili wa watu wote. Kama Asemavyo Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala):  
  
(( الَر كِتَابٌ أَنزَلْنَاهُ إِلَيْكَ لِتُخْرِجَ النَّاسَ مِنَ الظُّلُمَاتِ إِلَى النُّورِ بِإِذْنِ رَبِّهِمْ إِلَى صِرَاطِ الْعَزِيزِ الْحَمِيدِ ))

((Alif Lam Ra. (A.L.R.) Hichi ni Kitabu Tulichokiteremsha kwako ili uwatowe watu kwenye giza uwapeleke kwenye muangaza, kwa idhini ya Mola wao Mlezi, uwafikishe kwenye Njia ya Mwenye nguvu, Msifiwa)) [Ibraahiym: 1]


MAJINA YA QUR-AAN


Maulamaa na Wafasiri wa Qur-aan wametaja majina mengi ya Qur-aan kutokana na dalili katika Qur-aan yenyewe na pia Hadiythi Sharifu. Yafuatayo ni baadhi tu ya majina hayo:



KITABU

 (( ذَلِكَ الْكِتَابُ لاَ رَيْبَ فِيهِ هُدًى لِّلْمُتَّقِينَ))
((Hiki ni Kitabu kisichokuwa na shaka ndani yake; ni uongofu kwa wachamungu)) [Al-Baqarah: 2]





AL-FURQAAN (Upambanuzi)


(( تَبَارَكَ الَّذِي نَزَّلَ الْفُرْقَانَ عَلَى عَبْدِهِ لِيَكُونَ لِلْعَالَمِينَ نَذِيرًا ))

((Ametukuka Aliyeteremsha Furqani kwa mja wake, ili awe mwonyaji kwa walimwengu wote)) [Al-Furqaan: 1]




ADH-DHIKR (Ukumbusho)

))وَهَذَا ذِكْرٌ مُّبَارَكٌ أَنزَلْنَاهُ أَفَأَنتُمْ لَهُ مُنكِرُونَ((
((Na haya ni makumbusho yaliyobarikiwa, Tuliyoyateremsha. Basi je! Mnayakataa?)  [Al-Anbiyaa: 50]




AN-NUUR  (Mwangaza)

))يَا أَيُّهَا النَّاسُ قَدْ جَاءكُم بُرْهَانٌ مِّن رَّبِّكُمْ وَأَنزَلْنَا إِلَيْكُمْ نُورًا مُّبِينًا))

((Enyi watu! Umekufikieni ushahidi kutoka kwa Mola wenu Mlezi. Na Tumekuteremshieni Nuru iliyo wazi)) [An-Nisaa: 174]





MAWAIDHA

((يَا أَيُّهَا النَّاسُ قَدْ جَاءتْكُم مَّوْعِظَةٌ مِّن رَّبِّكُمْ وَشِفَاء لِّمَا فِي الصُّدُورِ وَهُدًى وَرَحْمَةٌ لِّلْمُؤْمِنِينَ))
((Enyi watu! Yamekujieni mawaidha kutoka kwa Mola wenu Mlezi, na poza kuponyesha yaliyomo vifuani, na uongofu, na rehema kwa Waumini)) [Yuunus: 57]




ALLAAH (SUBHAANAHU WA TA'ALA) AMEIHIFADHI QUR-AAN 


Bila ya shaka Qur-aan ni kitabu kitukufu kabisa anachokihitajia kila mtu kumpatia uongofu kamili awe katika njia iliyonyooka na awe katika Twa'a ya Mola Wake Mtukufu.  Naye Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) Ametuhakikishia kuhifadhiwa na kuthibitika kwake ili isiongezeke au kupungua hata neno au herufi moja ikaja ikawa hii Qur-aan imechanganyika na maneno ya mtu bali, ibakie kuwa ni maneno Yake Pekee Mola wa viumbe vyote.

Amesema Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala)    
))إِنَّا نَحْنُ نَزَّلْنَا الذِّكْرَ وَإِنَّا لَهُ لَحَافِظُونَ((

((Hakika Sisi ndio Tulioteremsha Ukumbusho huu, na hakika Sisi ndio Tutaokaoulinda)) [Al-Hijr: 9]
))إِنَّ الَّذِينَ كَفَرُوا بِالذِّكْرِ لَمَّا جَاءهُمْ وَإِنَّهُ لَكِتَابٌ عَزِيزٌ((
))لاَ يَأْتِيهِ الْبَاطِلُ مِن بَيْنِ يَدَيْهِ وَلَا مِنْ خَلْفِهِ تَنزِيلٌ مِّنْ حَكِيمٍ حَمِيدٍ((

((Kwa hakika wanayoyakataa mawaidha haya yanapowajia (wataangamia), na haya bila ya shaka ni Kitabu chenye nguvu na utukufu))
((Hautakifikia upotovu mbele yake wala nyuma yake. Kimeteremshwa na Mwenye hikima, Msifiwa)) [Fusswilat: 41-42]




KUTEREMSHWA QUR-AAN KATIKA RAMADHAAN


Anasema Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala)
   
))شَهْرُ رَمَضَانَ الَّذِيَ أُنزِلَ فِيهِ الْقُرْآنُ هُدًى لِّلنَّاسِ وَبَيِّنَاتٍ مِّنَ الْهُدَى وَالْفُرْقَانِ((
((Mwezi wa Ramadhaan ambao imeteremshwa humo Qur-aan kuwa ni uongofu kwa watu, na hoja zilizo wazi za uongofu na upambanuzi)) [Al-Baqarah: 184]




QUR-AAN IMETEREMSHWA KWA MITEREMSHO YA AINA MBILI KAMA IFUATAVYO:


MTEREMSHO WA MARA MOJA

Imeteremshwa Qur-aan kamili kutoka 'Lawhu-m-Mahfuudh' (Ubao uliohifadhiwa) mpaka mbingu ya kwanza. Kama inavyothibitishwa na kauli ya Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala): 

))إِنَّا أَنزَلْنَاهُ فِي لَيْلَةِ الْقَدْر((ِ
((Hakika Sisi Tumeiteremsha Qur-aan katika Laylatul Qadri, Usiku wa Cheo Kitukufu)) [Al-Qadar: 1]


)) إِنَّا أَنزَلْنَاهُ فِي لَيْلَةٍ مُّبَارَكَةٍ إِنَّا كُنَّا مُنذِرِينَ((
((Hakika Tumekiteremsha katika usiku uliobarikiwa. Hakika Sisi ni Waonyaji)) [Ad-Dukhaan: 3]



MTEREMSHO WA KIDOGO KIDOGO 


Imeteremshwa kwa muda wa miaka 23 tokea kupewa utume Mtume Muhammad (Swalla Allahu 'alayhi wa aalihi wa sallam)  hadi kufa kwake, nayo imeteremshwa kidogo kidogo kutokana na hali na matukio yaliyokuwa yakitokea.
Aayah za mwanzo kuteremshwa ni Aya tano katika Surat Al-'Alaq
بِسْمِ اللّهِ الرَّحْمَنِ الرَّحِيمِ  
))اقْرَأْ بِاسْمِ رَبِّكَ الَّذِي خَلَقَ ((
))خَلَقَ الْإِنسَانَ مِنْ عَلَقٍ((
)) اقْرَأْ وَرَبُّكَ الْأَكْرَمُ(( 
))الَّذِي عَلَّمَ بِالْقَلَمِ ((
))عَلَّمَ الْإِنسَانَ مَا لَمْ يَعْلَمْ  ((

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU
((Soma kwa jina la Mola wako Mlezi Aliyeumba))  
((Amemuumba binaadamu kwa tone la damu))
((Soma! Na Mola wako Mlezi ni Karimu kushinda wote!))
((Ambaye Amefundisha kwa kalamu))
((Kamfundisha mtu aliyokuwa hayajui))
[Al-'Alaq: 1-5]

Kutokana na rai zilizo za nguvu kabisa na zilizowafikiana zaidi, kwamba Aya ya mwisho kuteremshwa ni,

))وَاتَّقُوا يَوْمًا تُرْجَعُونَ فِيهِ إِلَى اللَّهِ ثُمَّ تُوَفَّى كُلُّ نَفْسٍ مَا كَسَبَتْ وَهُمْ لا يُظْلَمُونَ((
((Na iogopeni Siku ambayo mtarudishwa kwa Mwenyezi Mungu, kisha kila nafsi italipwa ilichochuma. Nao hawatadhulumiwa)) [Al-Baqarah: 281]



VIPI ILIKUWA IKITEREMSHWA QUR-AAN?


Kuteremeshwa Qur-aan katika kifua cha Mtume (Swalla Allahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) (Swalla Allahu 'alayhi wa aalihi wa sallam)  ilikuwa ni kutokana na 'Wahyi' (ufunuo) kama ilivyothibiti katika Qur-aan yenyewe.


))وَكَذَلِكَ أَوْحَيْنَا إِلَيْكَ قُرْآنًا عَرَبِيًّا لِّتُنذِرَ أُمَّ الْقُرَى وَمَنْ حَوْلَه()   


((Na namna hivi Tumekufunulia Qur-aan kwa Kiarabu ili uwaonye watu wa Mama wa Miji na walio pembezoni mwake))  [Ash-Shuura: 7]  

))نَحْنُ نَقُصُّ عَلَيْكَ أَحْسَنَ الْقَصَصِ بِمَا أَوْحَيْنَا إِلَيْكَ هَذَا الْقُرْآنَ وَإِن كُنتَ مِن قَبْلِهِ لَمِنَ الْغَافِلِينَ((

((Sisi Tunasimulia simulizi nzuri kwa kukufunulia Qur-aan hii. Na ijapokuwa kabla ya haya ulikuwa miongoni mwa wasiojua)) [Yuusuf: 3]

))اُتْلُ مَا أُوحِيَ إِلَيْكَ مِنَ الْكِتَابِ((

((Soma uliyofunuliwa katika Kitabu)) [Al-'Anqabuut: 45]






KWA NINI IMETEREMSHWA KIDOGO KIDOGO NA SIO UTEREMSHO MMOJA KAMILI?



Makafiri waliteta kuhusu Qur-aan kama ilivyo kawaida yao na ukaidi wao wa kukanusha kwa kila aina ya vitimbi na usemi, wakasema:


))وَقَالَ الَّذِينَ كَفَرُوا لَوْلَا نُزِّلَ عَلَيْهِ الْقُرْآنُ جُمْلَةً وَاحِدَة((

((Na wakasema waliokufuru: Kwa nini hakuteremshiwa Qur-aan kwa jumla moja?))   [Al-Furqaan: 32]


Wakikusudia kwa nini haikuteremshwa Qur-aan kama vitabu vya nyuma navyo ni Tawraah, Injiyl, Zabuur na kadhalika ambavyo viliteremshwa kwa jumla moja?


Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala)  Akawajibu kwa kuwapa Hikma Yake ya kuiteremsha kidogo kidogo kwa muda wa miaka ishirini na tatu kutokana na matukio na hali ilivyokuwa ikitokea,  kuwa ili Qur-aan ithibitike katika moyo wa Mtume (Swalla Allahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) kama aya ilivyomalizikia kusema.

))وَقَالَ الَّذِينَ كَفَرُوا لَوْلَا نُزِّلَ عَلَيْهِ الْقُرْآنُ جُمْلَةً وَاحِدَة كَذَلِكَ لِنُثَبِّتَ بِهِ فُؤَادَكَ وَرَتَّلْنَاهُ تَرْتِيلًا ((

((Na wakasema waliokufuru: Kwa nini hakuteremshiwa Qur-aan kwa jumla moja? Hayo ni hivyo ili tuuthibitishe moyo wako, na ndio tumeisoma kwa mafungu)) [Al-Furqaan: 32]


Vile vile Amesema Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala)    

))وَقُرْآناً فَرَقْنَاهُ لِتَقْرَأَهُ عَلَى النَّاسِ عَلَى مُكْثٍ وَنَزَّلْنَاهُ تَنزِيلاً((

((Na Qur-aan Tumeigawanya sehemu mbali mbali ili uwasomee watu kwa kituo, na Tumeiteremsha kidogo kidogo)) [Al-Israa: 106]