Friday, June 15, 2012

Mungu Wao Ni Mpira

Zingatio La Wiki 'Abdun-Naaswir Hikmany Iwapo mwanaadamu anataka kuonekana mtu wa maajabu, basi aseme kwamba hana ushabiki wa mpira wala sie mfuasi wa timu yoyote. Hapo uwanja wa stihzai, lawama na matusi utafunguliwa dhidi yake. Kwa hakika mpira ni mfumo mwengine wa maisha, kwani ina ratiba yake na ushabiki wake ni kinyume kabisa na mfumo mzima wa Kiislamu. Tunapozungumzia mpira hatumaanishi yale mazoezi ambayo wanaume wengi wanayafanya. Hapa tunazungumza kuhusiana na mechi ambazo vijana kwa wazee wanazifuatilia kuliko hata Qur-aan na Sunnah yake. Ingawa kwa upande fulani hayo mazoezi ya mpira nayo pia yana walakin, kwani kivazi chake ni cha utupu, mazoezi yanafanywa hadi wakati wa Swalaah na kituko chengine ni kuwepo timu za wanawake. Muislamu atambue kuwa mwenye kuamini muongozo wa asiyekuwa Mtume Muhammad (Swalla Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam) na akaitakidi kwamba huo ndio muongozo ulio kamili kuliko muongozo wa Mtume, basi mtu huyo ni kafiri. Halikadhalika, ratiba za mpira haswa klabu za Uingereza na timu za taifa za Ulaya ni zenye kuzishughulisha akili za Waislamu. Akili ambazo zinashindwa kuhifadhi ya maana zikadumazwa kwa majina ya wachezaji na historia zao. Basi tambua kwamba kuikataa na kuipa mgongo diyn ya Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) na ukawa hujifunzi chochote katika diyn ni kutoka nje ya Uislamu. Naye Anasema Muumba wa Mbingu na Ardhi: {{Na ni nani dhalimu zaidi kuliko yule aliyekumbushwa Aayah za Mola wake kisha akazikataa. Hakika Sisi ni wenye kuchukua kisasi kwa watu wabaya.}} [As-Sajdah: 22] Kwaweza kuwa na ukweli fulani katika burudani hiyo ya mpira kwamba Muislamu hana starehe nyengine zaidi ya hiyo. Na kwa wapenzi wa mpira wanasema ni bora kuliko ushabiki wa pombe ama uzinifu. Hayo yametolewa na mashabiki wa mpira. Tunawaambia kwamba hakuna kitu chochote katika dunia hii ambacho ni kibaya kwa asilimia mia moja. Kila kitu kina madhara na manufaa yanayohusiana nacho. Hata hivyo, mtazamo wa Sharia’h ya Kiislamu, pamoja na mambo mengine, unajumuisha kupima uzito wa faida na hasara za vitu. Kwani tumeshuhudia kuwa ligi za mpira zina madhara mengi kuliko manufaa. Hii ni kwa dalili ya Tamko Lake Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala): {{Sema: “katika hivyo, mna madhara makubwa na manufaa kwa baadhi ya watu. Lakini madhara yake ni makubwa zaidi kuliko manufaa yake.”}} [Al-Baqarah: 219] Miongoni mwa madhara makubwa ya mpira ni kuwafanya Waislamu kurukwa na akili ikawa hata kutoleana salamu ni kazi ngumu kabisa. Utawakuta kwenye vigenge na hata kazini wakizozana kuhusu mechi hizo. Katika maajabu makubwa ni pale mshabiki wa mpira ambaye ni kijana wa miaka 29 alipoamua kujidhulumu nafsi yake kwa kujinyonga huko Embakasi, Nairobi – Kenya mnamo tarehe 06/05/09. Kisa na mkasa? Ati timu yake imeshindwa! Kiroja kikubwa ni kwamba hiyo mechi wenyewe ilichezwa Uingereza hali ya kuwa yeye yupo Kenya. Kama si wazimu ni nini?! Ni vyema Waislamu wakatafuta ya maana kuliko kupotezewa muda wao katika mambo yasiyokuwa na manufaa yoyote. Sio kaburini wala siku ya Hisabu ambayo Muislamu ataulizwa: "Ni ipi timu yako" au "Nitajie wachezaji wawili wa timu fulani na historia zao." Hilo halipo, isipokuwa jitayarishe na masuala haya: "Nani Mola wako" na "Nani Mtume wako". Na iwapo hayo masuala ni mepesi basi endelea kufanya istihzai na diyn yako uyaone ya mtema kuni. Tunamuomba Allaah (Subhaanahu wa Ta’ala) Atuongoze katika njia sahihi na Atughufurie madhambi yetu.

Thursday, June 7, 2012

Qur-aan Maana, Majina na Kuteremshwa Kwake

NINI MAANA YA QUR-AAN? 

Qur-aan ni maneno ya Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala)   yaliyoletwa kama 'Wahyi' (Ufunuo) kwa Mjumbe wa Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) na Mtume wa mwisho Muhammad (Swalla Allahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) yaliyoandikwa katika Misahafu, yanayorithiwa na vizazi kwa vizazi, yaliyonukuliwa kwa mapokezi mengi, kusoma kwake ni ibaada, ni yenye miujiza hata kama ni sura ndogo kabisa, na ni uongofu kamili wa watu wote. Kama Asemavyo Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala):  
  
(( الَر كِتَابٌ أَنزَلْنَاهُ إِلَيْكَ لِتُخْرِجَ النَّاسَ مِنَ الظُّلُمَاتِ إِلَى النُّورِ بِإِذْنِ رَبِّهِمْ إِلَى صِرَاطِ الْعَزِيزِ الْحَمِيدِ ))

((Alif Lam Ra. (A.L.R.) Hichi ni Kitabu Tulichokiteremsha kwako ili uwatowe watu kwenye giza uwapeleke kwenye muangaza, kwa idhini ya Mola wao Mlezi, uwafikishe kwenye Njia ya Mwenye nguvu, Msifiwa)) [Ibraahiym: 1]


MAJINA YA QUR-AAN


Maulamaa na Wafasiri wa Qur-aan wametaja majina mengi ya Qur-aan kutokana na dalili katika Qur-aan yenyewe na pia Hadiythi Sharifu. Yafuatayo ni baadhi tu ya majina hayo:



KITABU

 (( ذَلِكَ الْكِتَابُ لاَ رَيْبَ فِيهِ هُدًى لِّلْمُتَّقِينَ))
((Hiki ni Kitabu kisichokuwa na shaka ndani yake; ni uongofu kwa wachamungu)) [Al-Baqarah: 2]





AL-FURQAAN (Upambanuzi)


(( تَبَارَكَ الَّذِي نَزَّلَ الْفُرْقَانَ عَلَى عَبْدِهِ لِيَكُونَ لِلْعَالَمِينَ نَذِيرًا ))

((Ametukuka Aliyeteremsha Furqani kwa mja wake, ili awe mwonyaji kwa walimwengu wote)) [Al-Furqaan: 1]




ADH-DHIKR (Ukumbusho)

))وَهَذَا ذِكْرٌ مُّبَارَكٌ أَنزَلْنَاهُ أَفَأَنتُمْ لَهُ مُنكِرُونَ((
((Na haya ni makumbusho yaliyobarikiwa, Tuliyoyateremsha. Basi je! Mnayakataa?)  [Al-Anbiyaa: 50]




AN-NUUR  (Mwangaza)

))يَا أَيُّهَا النَّاسُ قَدْ جَاءكُم بُرْهَانٌ مِّن رَّبِّكُمْ وَأَنزَلْنَا إِلَيْكُمْ نُورًا مُّبِينًا))

((Enyi watu! Umekufikieni ushahidi kutoka kwa Mola wenu Mlezi. Na Tumekuteremshieni Nuru iliyo wazi)) [An-Nisaa: 174]





MAWAIDHA

((يَا أَيُّهَا النَّاسُ قَدْ جَاءتْكُم مَّوْعِظَةٌ مِّن رَّبِّكُمْ وَشِفَاء لِّمَا فِي الصُّدُورِ وَهُدًى وَرَحْمَةٌ لِّلْمُؤْمِنِينَ))
((Enyi watu! Yamekujieni mawaidha kutoka kwa Mola wenu Mlezi, na poza kuponyesha yaliyomo vifuani, na uongofu, na rehema kwa Waumini)) [Yuunus: 57]




ALLAAH (SUBHAANAHU WA TA'ALA) AMEIHIFADHI QUR-AAN 


Bila ya shaka Qur-aan ni kitabu kitukufu kabisa anachokihitajia kila mtu kumpatia uongofu kamili awe katika njia iliyonyooka na awe katika Twa'a ya Mola Wake Mtukufu.  Naye Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) Ametuhakikishia kuhifadhiwa na kuthibitika kwake ili isiongezeke au kupungua hata neno au herufi moja ikaja ikawa hii Qur-aan imechanganyika na maneno ya mtu bali, ibakie kuwa ni maneno Yake Pekee Mola wa viumbe vyote.

Amesema Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala)    
))إِنَّا نَحْنُ نَزَّلْنَا الذِّكْرَ وَإِنَّا لَهُ لَحَافِظُونَ((

((Hakika Sisi ndio Tulioteremsha Ukumbusho huu, na hakika Sisi ndio Tutaokaoulinda)) [Al-Hijr: 9]
))إِنَّ الَّذِينَ كَفَرُوا بِالذِّكْرِ لَمَّا جَاءهُمْ وَإِنَّهُ لَكِتَابٌ عَزِيزٌ((
))لاَ يَأْتِيهِ الْبَاطِلُ مِن بَيْنِ يَدَيْهِ وَلَا مِنْ خَلْفِهِ تَنزِيلٌ مِّنْ حَكِيمٍ حَمِيدٍ((

((Kwa hakika wanayoyakataa mawaidha haya yanapowajia (wataangamia), na haya bila ya shaka ni Kitabu chenye nguvu na utukufu))
((Hautakifikia upotovu mbele yake wala nyuma yake. Kimeteremshwa na Mwenye hikima, Msifiwa)) [Fusswilat: 41-42]




KUTEREMSHWA QUR-AAN KATIKA RAMADHAAN


Anasema Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala)
   
))شَهْرُ رَمَضَانَ الَّذِيَ أُنزِلَ فِيهِ الْقُرْآنُ هُدًى لِّلنَّاسِ وَبَيِّنَاتٍ مِّنَ الْهُدَى وَالْفُرْقَانِ((
((Mwezi wa Ramadhaan ambao imeteremshwa humo Qur-aan kuwa ni uongofu kwa watu, na hoja zilizo wazi za uongofu na upambanuzi)) [Al-Baqarah: 184]




QUR-AAN IMETEREMSHWA KWA MITEREMSHO YA AINA MBILI KAMA IFUATAVYO:


MTEREMSHO WA MARA MOJA

Imeteremshwa Qur-aan kamili kutoka 'Lawhu-m-Mahfuudh' (Ubao uliohifadhiwa) mpaka mbingu ya kwanza. Kama inavyothibitishwa na kauli ya Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala): 

))إِنَّا أَنزَلْنَاهُ فِي لَيْلَةِ الْقَدْر((ِ
((Hakika Sisi Tumeiteremsha Qur-aan katika Laylatul Qadri, Usiku wa Cheo Kitukufu)) [Al-Qadar: 1]


)) إِنَّا أَنزَلْنَاهُ فِي لَيْلَةٍ مُّبَارَكَةٍ إِنَّا كُنَّا مُنذِرِينَ((
((Hakika Tumekiteremsha katika usiku uliobarikiwa. Hakika Sisi ni Waonyaji)) [Ad-Dukhaan: 3]



MTEREMSHO WA KIDOGO KIDOGO 


Imeteremshwa kwa muda wa miaka 23 tokea kupewa utume Mtume Muhammad (Swalla Allahu 'alayhi wa aalihi wa sallam)  hadi kufa kwake, nayo imeteremshwa kidogo kidogo kutokana na hali na matukio yaliyokuwa yakitokea.
Aayah za mwanzo kuteremshwa ni Aya tano katika Surat Al-'Alaq
بِسْمِ اللّهِ الرَّحْمَنِ الرَّحِيمِ  
))اقْرَأْ بِاسْمِ رَبِّكَ الَّذِي خَلَقَ ((
))خَلَقَ الْإِنسَانَ مِنْ عَلَقٍ((
)) اقْرَأْ وَرَبُّكَ الْأَكْرَمُ(( 
))الَّذِي عَلَّمَ بِالْقَلَمِ ((
))عَلَّمَ الْإِنسَانَ مَا لَمْ يَعْلَمْ  ((

KWA JINA LA MWENYEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU
((Soma kwa jina la Mola wako Mlezi Aliyeumba))  
((Amemuumba binaadamu kwa tone la damu))
((Soma! Na Mola wako Mlezi ni Karimu kushinda wote!))
((Ambaye Amefundisha kwa kalamu))
((Kamfundisha mtu aliyokuwa hayajui))
[Al-'Alaq: 1-5]

Kutokana na rai zilizo za nguvu kabisa na zilizowafikiana zaidi, kwamba Aya ya mwisho kuteremshwa ni,

))وَاتَّقُوا يَوْمًا تُرْجَعُونَ فِيهِ إِلَى اللَّهِ ثُمَّ تُوَفَّى كُلُّ نَفْسٍ مَا كَسَبَتْ وَهُمْ لا يُظْلَمُونَ((
((Na iogopeni Siku ambayo mtarudishwa kwa Mwenyezi Mungu, kisha kila nafsi italipwa ilichochuma. Nao hawatadhulumiwa)) [Al-Baqarah: 281]



VIPI ILIKUWA IKITEREMSHWA QUR-AAN?


Kuteremeshwa Qur-aan katika kifua cha Mtume (Swalla Allahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) (Swalla Allahu 'alayhi wa aalihi wa sallam)  ilikuwa ni kutokana na 'Wahyi' (ufunuo) kama ilivyothibiti katika Qur-aan yenyewe.


))وَكَذَلِكَ أَوْحَيْنَا إِلَيْكَ قُرْآنًا عَرَبِيًّا لِّتُنذِرَ أُمَّ الْقُرَى وَمَنْ حَوْلَه()   


((Na namna hivi Tumekufunulia Qur-aan kwa Kiarabu ili uwaonye watu wa Mama wa Miji na walio pembezoni mwake))  [Ash-Shuura: 7]  

))نَحْنُ نَقُصُّ عَلَيْكَ أَحْسَنَ الْقَصَصِ بِمَا أَوْحَيْنَا إِلَيْكَ هَذَا الْقُرْآنَ وَإِن كُنتَ مِن قَبْلِهِ لَمِنَ الْغَافِلِينَ((

((Sisi Tunasimulia simulizi nzuri kwa kukufunulia Qur-aan hii. Na ijapokuwa kabla ya haya ulikuwa miongoni mwa wasiojua)) [Yuusuf: 3]

))اُتْلُ مَا أُوحِيَ إِلَيْكَ مِنَ الْكِتَابِ((

((Soma uliyofunuliwa katika Kitabu)) [Al-'Anqabuut: 45]






KWA NINI IMETEREMSHWA KIDOGO KIDOGO NA SIO UTEREMSHO MMOJA KAMILI?



Makafiri waliteta kuhusu Qur-aan kama ilivyo kawaida yao na ukaidi wao wa kukanusha kwa kila aina ya vitimbi na usemi, wakasema:


))وَقَالَ الَّذِينَ كَفَرُوا لَوْلَا نُزِّلَ عَلَيْهِ الْقُرْآنُ جُمْلَةً وَاحِدَة((

((Na wakasema waliokufuru: Kwa nini hakuteremshiwa Qur-aan kwa jumla moja?))   [Al-Furqaan: 32]


Wakikusudia kwa nini haikuteremshwa Qur-aan kama vitabu vya nyuma navyo ni Tawraah, Injiyl, Zabuur na kadhalika ambavyo viliteremshwa kwa jumla moja?


Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala)  Akawajibu kwa kuwapa Hikma Yake ya kuiteremsha kidogo kidogo kwa muda wa miaka ishirini na tatu kutokana na matukio na hali ilivyokuwa ikitokea,  kuwa ili Qur-aan ithibitike katika moyo wa Mtume (Swalla Allahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) kama aya ilivyomalizikia kusema.

))وَقَالَ الَّذِينَ كَفَرُوا لَوْلَا نُزِّلَ عَلَيْهِ الْقُرْآنُ جُمْلَةً وَاحِدَة كَذَلِكَ لِنُثَبِّتَ بِهِ فُؤَادَكَ وَرَتَّلْنَاهُ تَرْتِيلًا ((

((Na wakasema waliokufuru: Kwa nini hakuteremshiwa Qur-aan kwa jumla moja? Hayo ni hivyo ili tuuthibitishe moyo wako, na ndio tumeisoma kwa mafungu)) [Al-Furqaan: 32]


Vile vile Amesema Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala)    

))وَقُرْآناً فَرَقْنَاهُ لِتَقْرَأَهُ عَلَى النَّاسِ عَلَى مُكْثٍ وَنَزَّلْنَاهُ تَنزِيلاً((

((Na Qur-aan Tumeigawanya sehemu mbali mbali ili uwasomee watu kwa kituo, na Tumeiteremsha kidogo kidogo)) [Al-Israa: 106]